Mdude Chadema: Nilitekwa kwa sababu za kisiasa

Mdude chadema akizungumza na wanahabari kuhusiana na kutekwa kwake.

Muktasari:

  • Mwanaharakati Mdude Nyagali  maarufu Mdude Chadema amehusisha kutekwa kwake na masuala ya siasa, akibainisha kuwa hana mpango wa kuhama Tanzania wala kuhofia kifo

Dar es Salaam. Mwanaharakati Mdude Nyagali  maarufu Mdude Chadema amehusisha kutekwa kwake na masuala ya siasa, akibainisha kuwa hana mpango wa kuhama Tanzania wala kuhofia kifo.

Mdude alitekwa Jumamosi ya Mei 4, 2019 Vwawa-Mbozi mkoani Songwe  na kupatikana Alhamisi Mei 9 eneo la Inyala Mbeya vijijini akiwa hoi.

Akizungumza na waandishi  wa habari leo Jumatatu Mei 20, 2019 jijini Dar es Salaam, Mdude amesema  yeye ni Mtanzania na hawezi kukimbia nchi huku akihusisha  kutekwa kwake na ukosoaji wa masuala mbalimbali mitandaoni.

“Ninachojua nilitekwa kwa sababu ya itikadi za kisiasa ila kwa kuwa mimi ni Mtanzania siwezi kuhama nchi kwa sababu ya hofu. Nitaendelea kuvumilia mpaka mwisho kama Yesu,” amesema Mdude.

Katika mkutano huo na wanahabari Mdude alimwaga machozi wakati akizungumzia namna alivyojikuta yupo porini baada ya waliomteka kumtupa.

“Nilijiuliza kosa langu ni lipi katika nchi hii na kama nina kosa mahakama si zipo kwa nini nifanyiwe hivi,” amesema Mdude huku akilia.