Meya Ubungo aeleza jinsi ya kukwepa foleni Ubungo-Mbezi

Muktasari:

Meya wa Ubungo, Boniface Jacob amewataka watumiaji wa barabara ya Morogoro kutumia njia mbadala za magari madogo kushoto na kulia mwa barabara ya Morogoro ili kukwepa foleni

Dar es Salaam. Meya wa Ubungo, Boniface Jacob amewataka watumiaji wa barabara ya Morogoro kutumia njia mbadala za magari madogo kushoto na kulia mwa barabara ya Morogoro ili kukwepa foleni.

Mbali na kutoa mbadala wa njia hizo, pia amewataka madereva kutotumia njia ya magari wanayopishana nayo ili kuepuka kuzuia magari mengine na kusababisha foleni kuwa kubwa.

Ametoa ujumbe huo leo Jumapili Mei 12, akisema  

foleni kubwa inatokana na mradi wa ujenzi wa barabara nane na mvua zinazoendelea kunyesha hasa wakati wa asubuhi na jioni.

“Ukifika Kimara kama unaenda Mbezi ingia kushoto baada ya Round about (mzunguko) ya Kimara utaenda na njia ya changarawe (service road) mpaka Mbezi Darajani ndiyo utarudi barabara kuu ya Morogoro,” amesema.

 Jacob amesema kwa wanaotoka Kibamba, Kwembe na Kibaha wakipita daraja la Kibamba kuna ‘service road’ za magari madogo za changarawe ambapo wakizitumia watasogea mpaka Mbezi Mwisho katika ujenzi wa daraja na kuingia barabara kuu ya Morogoro

“Kwa watu wanaotoka Kibamba kupita Mbezi kwenda Ubungo msirudi  tena barabara ya Morogoro bali tumieni njia ya Goba mtokee Makongo Juu, Changanyikeni au Mlimani City kwa dakika isiyozidi 20.”

“Ila Kwa watumiaji wa barabara ya Morogoro mnaotaka kutokea barabara Goba kwenda Mbezi Beach mnaweza kutumia njia ya Kibwegere kupitia Kibweheri na kisha Mpiji Magoe mpate kuikamata njia ya Mbezi Makabe kirahisi, njia hii pia wanaweza kuitumia wanaoelekea kwenda Bunju na Boko (barabara ya bagamoyo) kwa kupitia msitu wa Mabwepande haitazidi dakika 60 na napendekeza muitumie mchana tu.”

Watumiaji wa barabara ya Morogoro wanaokwenda Tabata amesema wanaweza kutumia njia ya Mbezi Mwisho kupitia Msigani  kupitia Kifuru kwenda Kinyerezi Mwisho bila ya kulazimika kurudi mpaka Kimara Mwisho kukutana na foleni.