Mhariri MCL asema wanawake wanaweza bila kuwezeshwa

Muktasari:

Mhariri Mtendaji Mkuu wa Mwananchi Communications Ltd (MCL), Bakari Machumu amezungumzia siku ya mwanamke duniani inayoadhimishwa kesho akisema dhana ya mwanamke akiwezeshwa anaweza haina tija kwani mwanamke anaweza pasi na kuwezeshwa

MCL ni kampuni inachapisha magazeti ya Mwananchi, The Citizen, MwanaSpoti na MCl Digital


Dar es Salam. Mhariri Mtendaji Mkuu wa Mwananchi Communications Ltd (MCL), Bakari Machumu amesema dhana ya ‘mwanamke akiwezeshwa anaweza’ inapaswa kuachwa kwa sababu inaonyesha hawezi kujitegemea mpaka akibebwa.

Katika salamu zake kuelekea siku ya wanawake duniani ambayo hufanyika Machi 8 kila mwaka, Machumu amesema siyo kweli kwamba mwanamke anaweza akiwezeshwa.

Amesema amesoma na kufanya kazi na wanawake wengi ambao wakati mwingine hufanya vizuri zaidi ya wanaume hivyo ibaki tu kuwa mwanamke anaweza.

“Siku ya wanawake duniani mimi sio mshabiki wa dhana ya wanawake wakiwezeshwa wanaweza, nimesoma na kufanya kazi na wanawake ninachokutana nacho ni uwezo mkubwa na wanatushinda. Nadhani wanawake wanaweza,” amesema .

Mhariri Mtendaji Mkuu huyo wa MCL amesema kinachotakiwa kufanywa ni uwapo wa mazingira sawa ya watoto wa kike na kiume kupata elimu kama fursa ya kufikia mafanikio yao.

“Dhana ya wakiwezeshwa inalemaza, inasukuma dhana kuwa hawezi kujitegemea na wanatakiwa kubebwa. Wanawake wanaweza,” amesema