Mkurugenzi Azam Media achaguliwa mjumbe bodi ya wakurugenzi CRDB

Baadhi wanahisa wakimpongeza Abdul Mohammed

Muktasari:

Mkurugenzi wa Masoko na Mauzo wa Azam Media Ltd, Abdul Mohammed leo Jumamosi Mei 18, 2019 amechaguliwa kuwa mjumbe wa bodi ya wakurugenzi wa Benki ya CRDB

Arusha. Mkurugenzi wa Masoko na Mauzo wa Azam Media Ltd, Abdul Mohammed leo Jumamosi Mei 18, 2019 amechaguliwa kuwa mjumbe wa bodi ya wakurugenzi wa Benki ya CRDB.

Abdul ambaye pia ni ofisa mtendaji mkuu wa timu ya mpira wa miguu ya Azam FC amechaguliwa baada ya kupata asilimia 16.86 ya kura za wanahisa wa benki ya CRDB.

Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo mwenyekiti wa kikao cha wanahisa jijini Arusha  Jaji mkuu mstaafu,  Augustine Ramadhani amesema wengine waliochaguliwa  ni  Ally Hussein Laay.

Laay, aliyekuwa mwenyekiti bodi iliyopita alipata  asilimia 27.52  ya kula. Wengine waliochaguliwa ni Martin  Warioba aliyepata asilimia 50.62 ya kura na Boniface Mahegi aliyepata  asilimia 27.42.

Wagombea 16 walishiriki uchaguzi huo katika makundi tofauti kulingana na viwango vya hisa.

Mkurugenzi mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela  amewapongeza  wajumbe hao kwa kuchaguliwa na kuahidi  kuwapa ushirikiano  kufanikisha benki hiyo kuendelea kuongoza nchini.