TAMTHILIA YA SULTAN: Mwasiti Rashid aliyeigiza sauti ya Dilsah Hatun

Muktasari:

  • Ni tamthilia inayohusu maisha ya Sultan Suleyman. Katika umri wa miaka 26 alianza mbio za kuitengeneza himaya yake ya Ottoman akitaka iwe kubwa kuliko ya Alexander the Great.

Dilsah Hatun

Alicheza kama Victoria lakini alibadilishwa jina na mama Sultan na kuitwa Dilsah Hatun, nafasi iliyochezwa na Reyhan Tasoren.

Katika tamthilia hii anaigiza kama dada ambaye alitoka nchi nyingine kwenda himaya ya Ottoman kwa ajili ya kulipiza kisasi. Akiwa huko pia alipata mchumba aliyeitwa Matrakcı Nasuh na kujaribu kumtumia kumuua Mfalme Sultan lakini alikuja kugundulika na kupewa kipigo cha kufa mtu na mumewe kupewa kazi ya kumuua hivyo aliamua kwenda kumtupa baharini na hapo ndio ikawa mwisho wake.

Nafasi nyingine aliyoinakilisha ni ya mama yake Hellena, mtoto wake Hellena alitaka kuolewa na Sehzade Mustafa alipokwenda kijijini Manisa japokuwa ndoa hiyo haikufanyika na huo ndio ukawa mwanzo wa mama Hellena naye kutoonekana tena katika tamthilia hiyo.

Mwasiti Rashid

Mwasiti ni msanii wa kuingiza sauti na ndiye aliyenakilisha sauti ya Sadca Hatun na Mama Hellena. Japokuwa kwa sasa katika tamthilia hiyo baada ya kufa kwa Sadca amekuwa akifanya kazi za wahusika ambao wanakuja na kuondoka.

Changamoto ambayo anasema anakabiliana nayo katika kunakilisha sauti ni pamoja na majina magumu ya wahusika wa tamthilia hiyo.

“Mashabiki wa tamthilia hiyo wanapokujua kuwa unaigiza sauti ya mhusika fulani ambaye ana tabia zisizoipendeza kwenye jamii, wanakuchukia,” anasema.

Kitaaluma anasema ni mcheza ngoma, muigizaji michezo ya redio na alishawahi kufanya matangazo mbalimbali ikiwamo la uzazi wa mpango.

Pia, anasema kwamba hufanya kazi ya ujasiriamali na anachoshukuru pamoja na kazi hiyo aliyoipata ya kunakilisha sauti hupata muda pia wa kwenda kusimamia biashara yake kwa kuwa siyo kazi ya kumfanya akae siku nzima kazini.

Anaeleza kuwa kutokana na namna wanavyofanya kazi, ni rahisi kama mtoto wa kike ukiamua kujichanganya kufanya kazi nyingine.