VIDEO: Mwendokasi yaichana katikati gari ndogo, dereva afariki papo hapo

Muktasari:

Basi la mwendokasi limegongana na gari dogo aina ya Nissan March eneo la Magomeni na kusababisha kifo cha dereva.

Dar es Salaam. Basi la mwendokasi lililokuwa likitoka maeneo ya Kariakoo kwenda Kimara, limeligonga gari dogo aina ya Nissan March na kukatika katikati  huku dereva  wa gari hilo dogo akifariki dunia papo hapo.

Ajali hiyo imetokea mchana wa leo Ijumaa Aprili 19,2019 eneo la Magomeni Mapima.

Shuhuda wa ajali hiyo, Issa Abdallah amesema mwenye gari dogo alikuwa anakata kona kutoka Magomeni kwenda Kariakoo, sasa wakati anataka kuikata kona katika taa ndogo za kuongoza magari za Magomeni Mapipa ambazo zilikuwa haziwaki ndipo gari dogo ikachelewa kupita na mwendokasi likawa limefika na kuligonga.

“Baada ya kumpitia, Mwendokasi ikaichana gari katikati na dereva kufariki pale pale,” amesema Abdallah.

Amesema vipande viwili vya gari hilo vimechukuliwa na kupelekwa kituo cha Polisi Magomeni huku mwili wa dereva huyo ambaye haujafahamika jina lake umepelekwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).

Amesema ajali hiyo imesababisha basi la Mwendokasi kuharibika kidogo pembeni mwa mlango upande wa kushoto. Baada ya hapo lilitoka nje ya barabara yake hali iliyosababisha njia hiyo kutopitika na jitihada za kulisogeza zilikuwa zinaendelea.

Polisi wameonekana hapo lakini hawakuwa tayari kuzunguza.

Endelea kufuatilia habari hii