Mwenge wapokewa Dodoma Mjini, kuzindua miradi saba maendeleo ya Sh11.6 bilioni

Muktasari:

Mwenge wa uhuru umepokelewa leo jijini Dodoma, utakagua miradi saba yenye thamani ya Sh11.6bilioni.

Dodoma. Mwenge wa Uhuru umekabidhiwa Wilaya ya Dodoma Mjini, leo Jumatano Agosti 14, 2019.

Miradi saba yenye thamani ya Sh11.6 bilioni itakaguliwa, kuzinduliwa na kukaguliwa na Mwenge huo.

Unakabidhiwa ukitoka Wilaya ya Chamwino, ikiwa tayari umeshakimbizwa za Mpwapwa na Kongwa tangu uingie mkoani Dodoma ukitokea mkoani Morogoro.

Akizungumza leo asubuhi, mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Patrobas Katambi amesema Mwenge huo utakimbizwa kilometa 184 katika wilaya hiyo.

“Miradi mitatu itawekewa jiwe la msingi, mmoja utatembelewa na mitatu itakaguliwa,” amesema Katambi.

Akikabidhi Mwenge huo Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Vumilia Nyamoga amesema jumla ya miradi mitano yenye thamani Sh626.5 milioni.

Amesema Mwenge huo, ulikimbizwa katika umbali wa Kilometa 176 katika vijiji 13 vya wilaya hiyo.

Awali kiongozi wa mbio za Mwenge Taifa Mzee Mkongea Ali ameitaka halmashauri ya Dodoma mjini kuwa na taarifa zote za miradi itakayokaguliwa na Mwenge huo na kuhakikisha watalaam wanaohusika wanakuwepo katika maeneo ya mradi.

" Mwenge wa uhuru hauonei mtu untenda haki kwa kwa watu wote, " amesema.