Mwenyekiti mpya wa CCM Iringa huyu hapa

Muktasari:

  • Wajumbe wa Kamati Kuu maalum ya CCM Mkoa wa Iringa wamemchagua Abel Nyamhanga kuwa mwenyekiti mpya wa chama hicho tawala mkoani humo baada ya kupata kura 318 kati ya kura 548

Iringa. Wajumbe wa Kamati Kuu maalum ya CCM Mkoa wa Iringa wamemchagua Abel Nyamhanga kuwa mwenyekiti mpya wa chama hicho tawala mkoani humo baada ya kupata kura 318 kati ya kura 548.

Uchaguzi huo umefanyika leo Jumapili Januari 6, 2019 mjini Iringa na kusimamiwa na mlezi wa CCM Mkoa wa Iringa, Waziri Mkuu mstaafu Mizengo Pinda.

Katika uchaguzi huo, wagombea wengine,  Aman Mwamwindi  alipata kura 224. Hata hivyo, uchaguzi huo ulifanyika mara mbili baada ya mara ya kwanza Nyamhanga na Mwamwindi wote kupata kura 224 huku mgombea mwingine, Vitus Mushi akipata kura 77.

Matokeo ya uchaguzi huo yalitangazwa na mwenyekiti wa uchaguzi huo, William Lukuvi na kuibua shangwe miongoni mwa wajumbe.

Nyamahanga anachukua nafasi ya aliyekuwa mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Iringa, Albert Chalamila ambaye aliteuliwa kuwa mkuu wa Mkoa wa Mbeya.