Mwingira amweleza Magufuli anavyochukizwa na amri za Ma-DC

Kiongozi wa Kanisa la Efatha, Mtume Josephat Mwingira

Muktasari:

  • Kiongozi wa Kanisa la Efatha, Mtume Josephat Mwingira amesema vitendo vinavyofanywa na wakuu wa wilaya kuwaweka watu ndani havina tija kwa jamii na utawala bora

Dar es Salaam. Kiongozi wa Kanisa la Efatha, Mtume Josephat Mwingira amewataka wakuu wa wilaya kupunguza mamlaka ya kutoa amri za kuweka watu ndani kwa kuwa hiyo inaweza kusababisha wananchi kuiona Serikali ni mbaya.

Mtume Mwingira ametoa rai hiyo leo Ikulu jijini Dar es Salaam wakati akitoa mchango wake wa mawazo kwenye mkutano maalum wa Rais Magufuli na viongozi wa madhehebu mbalimbali ya dini nchini.

Amesema viongozi hao wa wilaya wamejipa mamlaka ya kupitiliza kwa kuwakamata watu na kuwaweka ndani, akitolea mfano wachungaji wa kanisa lake wawili ambao amedai wameshawahi kukamatwa.

“La tatu ni la viongozi wetu wa wilaya, wanatoa amri ya kutia watu lokapu, ningeomba viongozi wetu wa wilaya wasiwe na mamlaka hayo, wamevuka mno, wameenda mbali mmo.”

“Unamuweka tu ndani halafu badaye humfungulii mashtaka wala nini, unamuacha unaenda umemdhalilisha mi naona kama wanaidhalilisha Serikali.”

 “Wakamkamata mchungaji wangu wa kwanza wakamtia ndani, nikauliza mkuu wa mkoa inakuwaje (bila kumtaja mkuu wa mkoa aliyemuuliza) mkuu wa mkoa akampigia simu mkuu wa wilaya akamuachia.”

“Unamuweka mtumishi wa Mungu ndani, haya mwingine ni yule wa Sengerema akamuweka mchungaji wangu ndani, nikamuuliza aniambie ee nimemuweka, nikamuuliza unataka tuione Serikali yetu ni mbaya au?”   amesema huku akimuahidi Rais Magufuli kuwa jambo jingine ataongea naye akipata nafasi ya kukutana naye.

Mkutano huo unaoendelea Ikulu umeitishwa na Rais Magufuli kujadili masuala mbalimbali ya kitaifa na viongozi wa dini.