Ndugai akumbuka ukarimu, kujitoa kwa Mengi

Spika wa Bunge, Job Ndugai

Muktasari:

  • Spika wa Bunge, Job Ndugai amemkumbuka mwenyekiti mtendaji wa IPP, Reginald Mengi kwa moyo wake wa kujitoa kwa jamii bila kujali hadhi aliyokuwa nayo

Dodoma. Spika wa Bunge, Job Ndugai amemkumbuka mwenyekiti wa kampuni za IPP, Reginald Mengi kwa moyo wake wa kujitoa kwa jamii bila kujali hadhi  aliyokuwa nayo.

Ndugai amesema hayo leo Ijumaa Mei 3 wakati wa kuanza kwa kikao cha Bunge jijini Dodoma alipokuwa akiwatangazia wabunge kuhusu kifo cha mfanyabiashara huyo na kueleza jinsi alivyoshirikiana na mhimili huo wa kutunga sheria.

Amesema kila alipoweza Mengi alishirikiana na Bunge kwenye maeneo tofauti yanayolenga kutatua kero za jamii na kuchangia kadri alivyoweza kufanikisha kinachotarajiwa kufanyika.

“Hivi karibuni alituchangia Sh50 milioni kwa ajili ya ujenzi wa vyoo vya mfano kwa kila jimbo. Mengi alikuwa mfanyabiashara na mwekezaji mkubwa nchini ambaye alijitoa kwa jamii kwa kiasi kikubwa. Mradi huu uliobuniwa na wabunge wanawake alisaidia kuuwezesha,”  amesema Ndugai.