Ofisa uvuvi mbaroni akituhumiwa kupokea rushwa

Muktasari:

  • Takukuru mkoani Mwanza inamshikilia ofisa uvuvi manispaa ya Ilemela, Williadius Buberwa kwa tuhuma za kupokea rushwa ya Sh1.5milioni

Mwanza. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoani Mwanza inamshikilia ofisa uvuvi wa manispaa ya Ilemela, Williadius Buberwa (33) kwa tuhuma za kupokea rushwa ya Sh1.5milioni.

Imeelezwa kuwa kitendo hicho ni kinyume na kifungu cha 15(1) cha sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumanne Desemba 4, 2018 naibu mkuu wa Takukuru mkoani Mwanza, Emmanuel Stenga amesema mtuhumiwa atafikishwa mahakamani muda wowote leo.

Stenga amesema  mtuhumiwa huyo alifanya doria isiyo rasmi katika eneo la Tunza wilayani Ilemela Oktoba 25, 2018 kwenye boti ya mfanyabiashara huyo ya kukuta ana vibali vyote.

Stenga amesema mtuhumiwa aliweka kikwazo, kuzuia samaki kushushwa na kutishia kuwataifisha endapo asingepewa fedha.

 “Aliomba rushwa ya Sh 2milioni ila mfanyabiashara huyo aliomba kiwango kipungue na kufika  Sh1.5milioni. Alipopewa fedha ndio akaruhusu mzigo kupakiwa kwenye gari,” amesema Stenga.