Pinda awapiga vijembe wanaotaka urais CCM

Muktasari:

Waziri Mkuu wa zamani wa Tanzania, Mizengo Pinda amesema hakuna mwanachama wa CCM mwenye haki ya kugombea urais mwaka 2020 na wanaohangaika kuusaka wana vitu vinawasumbua

Dodoma. Waziri Mkuu wa zamani wa Tanzania, Mizengo Pinda amesema hakuna mwanachama wa CCM mwenye haki ya kugombea urais mwaka 2020 na wanaohangaika kuusaka wana vitu vinawasumbua.

Pinda ametoa kauli hiyo leo Jumanne Julai 23, 2019 katika uzinduzi wa mradi wa vibanda vya biashara wa CCM katika hafla iliyohudhuriwa na katibu mkuu wa chama hicho, Dk Bashiru Ally.

Amesema anasikia kuna mtu anatapatapa kutaka urais kwa tiketi ya CCM, kusisitiza kuwa kwa muundo wa chama hicho tawala ulivyo, jambo hilo haliwezekani.

"Nimefanya kazi na Julius Nyerere miaka nane, mzee Mwinyi (Ali Hassan-Rais wa Awamu ya Pili) miaka 10, nimefanya kazi na Mkapa (Benjamin- Rais wa Awamu ya Tatu) miaka 10 lakini sijaona wala kusikia kinachojitokeza sasa,” amesema Pinda.

Amefafanua kuwa Magufuli anaelekea kumaliza miaka mitano ya awamu yake ya kwanza ya uongozi, kwa mujibu wa utaratibu za chama hicho anapaswa kuendelea na awamu ya pili na atakapomaliza lazima wana CCM wataanza kunong’ona pengine kutaka aongezewe muda.