VIDEO: Polisi Tanzania yaeleza itakavyoimarisha ulinzi mkutano wa SADC

Kamanda wa Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Mwalimu Julius Nyerereleo kuhusiana na hali ya usalama kuelekea Mkutano wa SADC. Picha na Anthony Siame

Muktasari:

Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam nchini Tanzania, Lazaro Mambosasa amesema licha ya baadhi ya barabara katikati ya jiji hilo zitafungwa ili kupisha mkutano wa 39 wa Jumuiya ya maendeleo kusini mwa Afrika (SADC), kuanzia kesho itaimarisha ulinzi kwa kutumia mbinu mbalimbali

Dar es Salaam. Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam nchini Tanzania limesema kuanzia kesho Jumatano litaimarisha ulinzi kwa kutumia vikosi vyote vya doria ikiwemo mbwa, farasi na helicopter ili kuhakikisha mkutano wa 39 Jumuiya ya maendeleo kusini mwa Afrika (SADC), unamalizika salama.

Doria hiyo inaanza kesho ambapo Tanzania itampokea kiongozi wa kwanza kuwasili, Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa.

Akizungumza na vyombo vya habari leo Agosti 13, 2019 jijini Dar es Salaam, Kamanda wa Kanda hiyo, Lazaro Mambosasa amesema doria hiyo ni sehemu ya maandalizi ya kuwapokea wakuu wa nchi 15 ambao wote wamedhibitisha kuhudhuria mkutano huo.

"Jeshi la Polisi kanda maalum Dar es salaam linatarajia kupokea wakuu wa nchi kuanzia Agosti 16, 2019, ulinzi utaimarishwa kuanzia mapokezi yao Airport, Hoteli wanazofikia na kuelekea katika kumbi za mikutano," amesema.

Amesema sambamba na hilo wanaendelea kukamata pikipiki zote na magari yanayovunja sheria na katazo la kuingia mjini ambapo jumla ya magari na pikipiki 126  zimechukuliwa hatua za kisheria.

"Madereva wengi wameendelea kutupa ushirikiano katika siku zote za mkutano huu wa jumuiya ya maendeleo ya nchi za kusini mwa jangwa la Sahara SADC, tunaomba wananchi wawe watulivu wakati misafara ya viongozi ikipita maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es salaam," amesema

Aidha Mambosasa amesema baadhi ya barabara katikati ya jiji la Dar es Salaam zitafungwa na kwamba barabara hizi zitatangazwa baadaye.