RC Arusha aagiza uchunguzi ugonjwa wa kuharisha

Muktasari:

  • Mkuu wa mkoa Arusha aagiza uchunguzi baada ya watu 310 kuripotiwa kuugua ugonjwa kwa kuharisha na kutapika Arusha. Mkuu wa mkoa huo, Mrisho Gambo awataka wataalam afya kuchunguza chanzo cha mlipuko wa ugonjwa wa kuharisha.

Arusha. Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo ameagiza maofisa afya mkoani hapa, kufanya uchunguzi juu ya mlipuko wa watu kupata ugonjwa wa kuharisha na kutapika uliowakumba watu katika jiji la Arusha.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Alhamisi Machi 14, 2019 baada ya kutembelea maeneo ambayo watu wameripotiwa kuugua, Gambo amesema uchunguzi wa kitaalam umebainisha maji yanayosambazwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira (Auwsa) ni salama.

Gambo amesema baada ya kusambazwa taarifa huenda maji ni tatizo, Auwsa na viongozi wa Bonde la Pangani wamefanya uchunguzi wa maabara na kubaini maji ya Auwsa ni salama.

Amesema ili kujua chanzo cha ugonjwa huo ameagiza maofisa wa afya kuendelea na uchunguzi kubaini chanjo cha ugonjwa huo.

Kaimu Mganga mkuu wa mkoa Arusha, Dk Omar Chande amesema watu 310 wameripotiwa kuugua ugonjwa wa kuhara na kutapika katika jiji la Arusha.

Dk Chande amesema uchunguzi wa awali uliofanyika baada ya kuchukuliwa sampuli za wagonjwa imebainika wameugua magonjwa ya matumbo.

"Tunaendelea na uchunguz,i maofisa wa afya wapo katika vituo vya afya kufanya uchunguzi lakini wote waliougua walipata tiba na kuruhusiwa hakuna aliyelazwa," alisema.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha, Jonathan Shani ameonya jeshi hilo litakamata mtu yeyote ambaye atatoa taarifa za uchochezi juu ya tukio hilo.

"Taarifa rasmi ya Serikali imetolewa kuwa maji si chanzo cha tatizo hivyo ambaye atatoa ama kusambaza taarifa potofu atachukuliwa hatua." Amesema.

Kwa upande wake mkurugenzi wa Auwsa, Luth Koya alisema mtandao wao wa maji upo salama licha ya kuendelea na mradi mkubwa wa uboreshaji maji katika jiji la Arusha.