RC amkalia kooni DED vitambulisho vya wajasiriamali, utata waibuka

Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Dk Binilith Mahenge

Muktasari:

Hata hivyo, mratibu wa ugawaji wa vitambulisho hivyo wilayani hapo, Christina Sam alisema tathmini iliyofanywa na halmashauri imeonyesha wajasiriamali wadogo waliopo ni 3,728, huku wakiwa wamepokea vitambulisho 12,000.

Dodoma. Wakati mkuu wa mkoa wa Dodoma, Dk Binilith Mahenge akimtaka mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Chamwino, Athuman Masasi kujieleza kwa kushindwa kufikia lengo la ugawaji wa vitambulisho kwa wafanyabiashara wadogo, imebainika idadi yao wilayani humo ni 3,728 wakati vilivyotolewa ni 12,000.

Dk Mahenge pia ameagiza watendaji wa kata wote na katibu tarafa ambao wameuza vitambulisho chini ya nusu ya walivyopewa waandikiwe barua ya kujieleza kwa nini wasichukuliwe hatua kwa kutotekeleza agizo la Rais John Magufuli.

Dk Mahenge alitoa agizo hilo wilayani hapo wakati akikagua idadi ya wajasiriamali waliokwishapatiwa vitambulisho sambamba na ugawaji wa vitambulisho hivyo kwa wakuu wa idara wa halmashauri.

Hata hivyo, mratibu wa ugawaji wa vitambulisho hivyo wilayani hapo, Christina Sam alisema tathmini iliyofanywa na halmashauri imeonyesha wajasiriamali wadogo waliopo ni 3,728, huku wakiwa wamepokea vitambulisho 12,000.

Alisema vitambulisho hivyo vimeanza kutumika vibaya kwa watu wasio waaminifu kwa kuazimishana na kudanganya uwezo wa mauzo yao, huku baadhi ya wafanyabaishara wa mifugo wakivitumia jambo ambalo linaweza kuathiri makusanyo.