VIDEO: Rais Magufuli awasili Malawi

Muktasari:

  • Rais John Magufuli amewasili mjini Lilongwe, Malawi kuanza ziara ya siku mbili nchini humo baada ya kupata mwaliko kutoka kwa Rais wan chi hiyo, Peter Mutharika.

Dar es Salaam. Rais John Magufuli amewasili salama katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kamuzu uliopo mjini Lilongwe nchini Malawi.

Rais Magufuli amewasili mjini Lilongwe leo Jumatano Aprili 24 ikiwa ni ziara yake i ya siku mbili nchini Malawi baada ya kupata mwaliko kutoka kwa mwenyeji wake, Rais Peter Mutharika.

Rais Magufuli ambaye ameambatana na mke wake, Mama Janeth waliwasili uwanjani hapo saa 11:18 asubuhi kwa kutumia ndege ya Shirika la Ndehe Tanzania (ATCL) na kupokelewa na mwenyeji wake, Rais Mutharika.

Baada ya Rais Magufuli kuwasili uwanjani hapo, nyimbo za Taifa za Tanzania na Malawi zilipigwa na kufuatiwa na Rais Magufuli kukagua gwaride lililoandaliwa kwa heshima yake.

Rais Magufuli ambaye yupo Malawi kwa ziara ya Serikali ya siku mbili anatarajiwa kuweka shada la maua katika mnara wa kumbukumbu ya aliyekuwa Rais wa  nchi hiyo, Hayati Bingu Mutharika.

Pia leo atafanya mazungumzo na mwenyeji wake Rais Mutharika na jioni atahudhuria dhifa ya kitaifa aliyoandaliwa na Rais huyo wa Malawi.

Rais Magufuli aliondoka katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Dar es Salam leo asubuhi na kuagwa na viongozi mbalimbali.