Rayvanny ajisalimisha Basata asubuhi hii

Muktasari:

Amefika katika ofisi za Baraza la Sanaa kwaajili ya mahojiano kuhusu wimbo wake mpya wa Mwanza


Dar es Salaam. Siku moja baada ya wimbo wake wa Mwanza kufungiwa, msanii Rayvanny amewasili katika Baraza la Sanaa la Taifa (Basata) asubuhi hii.

Rayvany aliwasili katika baraza hilo  saa 11:30 akiwa na gari jeupe aina ya  Harrier  akiwa ameambatana na watu wawili.

Akiwa amevalia suruali nyeusi na sweta la rangi ya machungwa yenye kofia, alijifunika usoni ili kukwepa kamera za wanahabari waliojazana katika ofisi za Baraza hilo zilizopo Ilala Bungoni jijini Dar es Salaam.

Baada ya kufika hapo aliegesha gari kwa muda kabla ya kuelekea ofisi za Katibu Mtendaji wa Baraza hilo, Godfrey Mngereza.

Kabla ya kufika katika ofisi za Baraza hilo, leo saa 3.15 asubuhi katika mtandao wa Instagram aliandika waraka mrefu wa utetezi wake kuhusu wimbo, Mwanza uliotoka siku tatu zilizopita.

Katika utetezi wake amesema wimbo huo umekusudia kutoa faraja kwa wakazi wa Mwanza baada ya hivi karibuni kutokea maafa ya kuzama kwa kivuko.

Ameongeza kuwa kila alichoimba kwenye wimbo huo kililenga kutoa mafunzo kwa jamii kujiepusha na vitendo viovu ikiwamo ngono na mavazi yasiyokubalika.