Safari za baharini Zanzibar zasitishwa

Muktasari:

  • Mamlaka ya Usafiri Baharini Zanzibar (ZMA) imesitisha usafiri pamoja na shughuli za uvuvi baharini kuanzia mchana huu kutokana na uwapo wa kimbunga.

Unguja. Mamlaka ya Usafiri Baharini Zanzibar (ZMA) imesitisha usafiri wa baharini kuanzia mchana huu kutokana na kuwapo tahadhari ya kutokea  kimbunga nchini.

Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari kutoka kwa kaimu mkurugenzi wa mamlaka hiyo, Ramadhan Hussein wamelazimika kusitisha safari kwa vyombo vyote baharini hadi pale taarifa zaidi za mamlaka ya hali ya hewa zitakapotolewa.

"Kwa kuwa tumepata taarifa za kuwapo kimbunga nchini na sisi kama ni sehemu ya Tanzania tumeona kuna umuhimu wa kusitisha safari zetu," amesema.

Amesema mbali ya kusitisha vyombo vya usafiri baharini, lakini pia anatoa wito kwa wavuvi nao kusitisha shughuli zao hadi hali ya utulivu itakaporejea.

Amesema lengo la kusitisha safari pamoja na shughuli za uvivu ni kuwanusuru wananchi mapema na janga la kimbunga ambalo linaweza kutokea.

Hussein alitoa wito kwa wananchi wote waliopo maeneo ya karibu na bahari ya hindi kufatilia pamoja na kufuata maagizo ya mamlaka hiyo pamoja na mamlaka ya hali ya hewa.