Selcom yawazawadia mamilioni washindi wa shinda mtaji

Muktasari:

  • wafanyabiashara sita wamejinyakulia mamilioni ya pesa  katika shindano la ‘Shinda Mtaji’ linaloratibiwa na kampuni ya Selcom na Mastercard inayolenga kukuza kuongeza kipato cha wafanyabiashara nchini.

Dar es Salaam. Wafanyabiashara sita wameibuka kidedea kwa kunyakua mamilioni ya fedha katika droo ya tatu ya promosheni ya ‘Shinda Mtaji’ inayoratibiwa na kampuni ya Selcom na Mastercard  kwa lengo la kuwaongezea mitaji na kukuza biashara zao.

Miongoni mwa wafanyabiashara hao waliojinyakulia Sh 1 milioni kila mmoja ni Faraji Suleiman ambaye anamiliki Faraji Hardware jijini Dar es Salaam na Gerald Moshi anayewakilisha kampuni ya Moshi Shop iliyopo Arusha.

Mshindi mwingine ni Balozi wa baa ya Liquid iliyopo Kurasini jijini Dar es Salaam, Piere Gumbo maarufu ‘Liquid master’ ambaye hivi karibuni amejizolea umaarufu mitandaoni kwa usemi wake ‘mamaa nakufaa’.

Promosheni hiyo iliyozinduliwa Novemba mwaka jana inalenga wafanyabiashara wote nchini ambao wanaendelea kujiunga na kutumia huduma ya Masterpass QR katika kupokea malipo mbalimbali kwenye maeneo yao ya biashara na wafanyabiashara ambao tayari wameshajiunga na huduma hiyo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana wakati wa kukabidhi hundi kwa washindi hao, meneja masoko wa Selcom, Juma Mgori alisema promosheni hiyo inamuwezesha mfanyabiashara kujishindia Sh 1 milioni kila wiki kwa muda wa miezi mitatu.