Serikali kuandaa sheria kupunguza umri wa kupima VVU

Muktasari:

Serikali inaandaa sheria kwa ajili ya kupunguza umri wa mtu kupima VVU kutoka wa sasa wa miaka 18 kwenda juu ili kuyafikia makundi lengwa ya umri wa chini ya miaka 18.


Dodoma. Serikali inaandaa sheria kwa ajili ya kupunguza umri wa mtu kupima Virusi vya Ukimwi (VVU) ili waweze kuyafikia makundi lengwa.

Akijibu swali la nyongeza bungeni leo Ijumaa Februari 1,

2019, Naibu Waziri wa Afya, Dk Faustine Ndugulile amesema mchakato wa kubadili sheria hiyo uko katika hatua za mwisho.

DK Ndugulile amesema sheria ya sasa inataka mtu anayepimwa VVU anatakiwa kuwa na umri wa kuanzia miaka 18 hivyo kundi kubwa linaachwa.

Katika swali la nyongeza mbunge wa Mtambile Masoud Abdallah Salim (CUF) amehoji ni lini Serikali itaelekeza nguvu zake katika kuwapima wanafunzi wa sekondari kwani nguvu inahitajika kwa vijana wa kuanzia miaka 15-24.

"Serikali tumeona tatizo katika sheria hiyo kwamba inatamka mtu mzima wa kuanzia miaka 18 ndiye anapaswa kupima virusi vya Ukimwi hivyo sheria mpya itashusha umri huo,"amesema Dk Ndugulile.

Katika swali la msingi mbunge huyo ameitaka Serikali kutangaza mkakati wa kampeni ya kupima VVU kwa Jiji la Dodoma kufikia mpango wa 90,90,90 kwani UKIMWI umeongezeka.