Serikali ya Tanzania yataifisha mali zenye thamani sh 93.16 bilioni

Makamu wa Rais, Samia Suluhu akizindua kitabu cha mwongozo wa utendaji kazi kwa Taasisi za kutaifisha mali zitokanazo na uhalifu (Arinsa) wakati wa ufunguzi wa mkutano wa maadhimisho ya miaka 10 ya ushirikiano wa taasisi hizo, jijini Dar es Salaam leo. Picha na Ericky Boniphace

Muktasari:

Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan amesema kuwa Tanzania imetaifisha mali zilizotokana na uhalifu zenye thamani ya Sh93.16 bilioni tangu mwaka 2009 Arinsa ilipoanzishwa.


Dar es Salaam. Tanzania imetaifisha mali zilizotokana na uhalifu zenye thamani ya jumla ya Sh93.16 bilioni ikiwa ni juhudi za ushirikiano wa Taasisi za kutaifisha mali zitokanazo na uhalifu Kusini mwa Afrika (Arinsa).

Hayo yamebainishwa leo Juni 12, jijini Dar es Salaam na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan wakati akifungua mkutano wa maadhimisho ya miaka 10 ya Arinsa uliozikutanisha nchi 16 wanachama wa umoja huo.

Mama Samia amesema fedha hizo zimepatikana kutokana na uhalifu kwenye madini, magari na pikipiki, upatu (Deci), mbao pamoja na mazao mengine ya misitu.

"Tanzania tumefanya mabadiliko ya sheria zetu ili tuweze kutaifisha mali zinazotokana na uhalifu na kuzuia utakatishaji wa fedha. Dhima ya Arinsa inakwenda sambamba na maono ya Rais John Magufuli katika kupambana na rushwa na ufisadi," amesema Makamu wa Rais.