Shahidi akwamisha kesi ya Zitto

Mbunge was Kigoma Mjini Zitto Kabwe akitoka katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu baada ya Kesi ya uchochezi kuahirishwa baada ya shahidi kushindwa kufika Mahakamani.

Muktasari:

  • Kesi ya uchochezi inayomkabili mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), Zitto Kabwe imeshindwa kuendelea katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kutokana na shahidi kutofika mahakamani

Dar es Salaam. Kesi ya uchochezi inayomkabili mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), Zitto Kabwe imeshindwa kuendelea katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kutokana na shahidi kutofika mahakamani.

Wakili wa Serikali, Nassoro Katuga amedai leo Jumanne Januari 29, 2019 mbele ya hakimu mkazi mkuu, Huruma Shahidi kuwa kesi hiyo ilipangwa kwa ajili ya kuanza kusikilizwa lakini amepata matatizo ya kifamilia na kushindwa kufika.

“Kwa jinsi  upande wa mashtaka tulivyokuwa tumejipanga tulitaka tuanze na ushahidi leo na shahidi tuliyekuwa tumemuandaa amepata matatizo ya kifamilia tunaomba kuahirishwa kwa muda,” amesema Katuga.

Wakili wa utetezi,  Jebra Kambole amedai mshtakiwa alikuwa amejiandaa kwa ajili ya kuanza kusikilizwa lakini pia ana majukumu mengine  kuomba tarehe za mwishoni.

Hakimu Shahidi baada ya kusikiliza maelezo hayo ameahirisha kesi hiyo hadi Februari 27, 2019  kwaajili ya kuanza kusikiliza mashahidi wa upande wa mashtaka.

Katika kesi ya msingi,  Zitto anadaiwa kutenda makosa hayo   Oktoba 28, 2018 katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika katika ofisi za  makao makuu ya chama cha ACT Wazalendo.

Alifikishwa katika mahakama hiyo na kushtakiwa kwa mashtaka matatu ya uchochezi.