Shahidi kesi ya dhahabu aieleza mahakama alivyolikamata gari

Muktasari:

Shahidi wa sita ameieleza mahakama jinsi alivyokwenda kukamata gari lililokuwa na shehena ya dhahabu lakini alipofika eneo la tukio akamkuta mkuu wake wa kazi  akamueleza kwamba tayari wameshaikamata hivyo alirudi ofisini.

Mwanza. Mkaguzi msaidizi wa kituo cha polisi cha Kamanga wilayani Sengerema,  Albert Malisa ambaye ni shahidi wa sita kwenye kesi ya kusafirisha shehena ya dhahabu, ameieleza mahakama jinsi alivyopokea maelezo kutoka kwa mkuu wake wa kazi kwenda kukamata gari lililokuwa limebeba dhahabu hiyo lakini alipofika eneo la tukio alielezwa kwamba tayari gari hilo limeshakamatwa.

Amedai kuwa Januari 5, mwaka huu saa 3:30 asubuhi, alipokea simu kutoka kwa OCD wa wilaya ya Sengerema, afande Makori akimueleza kwenda kuikamata gari aina ya Toyota Mark Two katika maegesho ya kivuko cha Mkombozi.

Amedai baada ya kupokea maelezo hayo aliwachukua askari wengine wawili wakiwa na silaha kwenda eneo la tukio.

“Tuliona kweli kuna gari la polisi na lingine dogo zikiwa kwenye yard hiyo zimepangana,” amesema shahidi huyo.

Amedai kuwa baada ya kuyasogelea magari hayo, walimkuta Afande Morisi Okinda (mshatakiwa wa tano, aliyekuwa mkuu wa operesheni mkoa wa Mwanza) akiwa kwenye gari la polisi kwa nyuma na dereva wake, koplo Kasala na afande Matete aliyeshuka kutoka kwenye ile gari ndogo kwa ajili ya kusalimiana.

Amedai baada ya kusalimiana alimueleza kilichompeleka pale kuwa ni kukamata gari dogo lakini akaambiwa na afande Okinda kwamba tayari gari hilo wameshalikamata.

Amedai baada ya kuambiwa hivyo, alirudi ofisini kwake na kumueleza OCD Makori kuhusu maelekezo aliyopewa baada ya kufika eneo la tukio.