Sirro: Njombe iko shwari

Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro

Muktasari:

Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro amewataka wananchi mkoani Njombe kuendelea na majukumu yao kwa kuwa watuhumiwa wa mauaji ya watoto wameshakamatwa


Dar es Salaam. Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro amewataka wananchi mkoani Njombe kuendelea na shughuli zao za kila siku kwa kuwa mji huo uko shwari.

IGP Sirro ametoa wito huo leo Jumatano 13, 2019 katika mahojiano ya Kipindi cha Jambo Tanzania kinachorushwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC).

Amesema kuwa ulinzi umeimarishwa mkoani humo hivyo wananchi waendelee na shughuli zao za kila siku bila wasiwasi.

 “Njombe ni shwari na itaendelea kuwa shwari, Watanzania wenzangu fanyeni kazi zenu maana tumetawanya polisi wa kutosha. Mzazi huna sababu ya kuhangaika kumpeleka mtoto shuleni, niwahakikishie kuwa mambo yako vizuri,” amesema Sirro

Amesema kuwa waliofanya mauaji hayo wameshakamatwa na watapelekwa mahakamani

 “Waliofanya matukio ya mauaji Njombe wote wamekamatwa, wengine utaona ilikuwa ni ugomvi wa familia, mtoto akaona baba mdogo ananichukia ngoja niue watoto wake, akaua watoto watatu” amesema Kamanda Sirro.

“Huyo mwingine anasema amepewa uchawi na babu yake, kwa hivyo anapata maluweluwe, huyu amekamatwa, akipata maluweluwe anajisikia anataka damu na anaua watoto. Ukiangalia matukio haya yanaanzia kwenye familia,” amesema.

Amesema hata mauaji ya watoto yaliyoripotiwa kutokea mkoani Simiyu yanahusiana na imani ya kishirikina.

 “Lakini pia hata hii ya Simiyu (mauaji) tumeshatuma watu wetu kule na yenyewe yameshaonekana ni ya kishirikina, tumewaomba watu wa Simiyu watupe taarifa ili tuwashughulikie,” amesema.

Jana Jumanne Februari 12, 2019 watuhumiwa watatu wa utekaji na mauaji ya watoto wilayani Njombe walifikishwa katika Mahakama ya hakimu mkazi Njombe, ikiwa ni mara ya kwanza kwa watuhumiwa mauaji hayo yaliyotikisa mkoani Njombe kuanzia Novemba 2018 kufikishwa mahakamani.