TFS yafunga mtambo kuchakata mazao ya nyuki Singida

Kaimu Meneja wa Wakala wa Huduma za Misitu wilaya ya Manyoni Juma Mchafu akimuonyesha mtambo wa kuchakata asali Mtendaji Mkuu wa TFS Profesa Dos Santos Silayo

Muktasari:

  • Singida yapata mtambo wa kuchakata asali, una uwezo wa kuchakata lita 500 kwa siku

Dar es Salaam. Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) imefunga mtambo wa kuchakata mazao ya nyuki wilayani Manyoni mkoani Singida wenye uwezo wa kuchakata asali lita 500 kwa siku.

Mtambo huo uliogharimu Sh80 milioni unatarajiwa kuondoa tatizo la ubora duni wa asali na nta katika ukanda huo na maeneo ya jirani.

Kaimu Meneja Mawasilino wa TFS, Tulizo Kilaga ameieleza Mwananchi leo Machi 14, 2019 kuwa mtambo huo umefungwa katika kiwanda cha wakala hao kilichopo Manyoni lakini pia wafugaji wa nje wataruhusiwa kuchakata mazao yao.

Amesema kiwanda  hicho kwa kiasi kikubwa kitategemea mali ghafi toka kwenye msitu wa Aghondi uliopo eneo la Itigi.

Amesema katika uvunaji wa awali wamefanikiwa kuvuna mizinga 459 kati ya 729 na kupata asali kilo 6,175 sawa na tani 6.175 wastani wa kilo 13.45 kwa mzinga.

“Takwimu hizo ni kulingana na tulizopata jana ila kwa kifupi kazi inaendelea na tunatarajia mafanikio makubwa makubwa kupitia mtambo huu,” amesema.