TTB kurudi China kusaka watalii

Muktasari:

  • Baada ya Novemba 2018, Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) iliratibu ziara ya kutangaza vivutio vya utalii vya Tanzania iliyofanyika katika miji ya Beijing, Shanghai, Chengdu, Guangzhou na Hong Kong kuleta watalii zaidi ya 10,000. Wameratibu ziara nyingine kwa lengo la kupata watalii wengi zaidi kutoka nchini humo.

Dar es Salaam. Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) itafanya tena misafara ya utangazaji utalii (roadshows) nchini China kwenye miji minne.

Lengo la safari hizo ni kuvuna watalii kama ambavyo walifanya mwaka 2018 ambapo watalii 10,000 kutoka nchini humo walitembelea Tanzania.

Akizungumza jana Jumatano Juni 12, 2019 na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa TTB, Jaji mstaafu Thomas Mihayo alisema misafara hiyo itaanza Juni 16 hadi 26, 2019 katika miji ya Beijing, Shanghai, Nanjig na Changsha.

Alifafanua wakiwa kwenye safari hiyo watashiriki maonyesho ya biashara na uchumi kati ya China na Afrika yatakayofanyika katika mji wa Changsha.

Naye Mkurugenzi mwendeshaji wa TT, Devota Mdachi alisema wanaishukuru Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kusimamia vema sheria za uhifadhi, kutoa miongozo ikiwamo ya kusimamia hifadhi kwa ajili ya kizazi kijacho.