Tabora Boy’s yataja sababu kushika nafasi ya tano matokeo kidato cha sita

Muktasari:

  • Shule kongwe ya Sekondari ya Wavulana Tabora, imejipanga kuwa ya kwanza mwakani na kuzidi kupunguza daraja la pili kwa lengo la kubakia na daraja la kwanza pekee katika mitihani yote ya Kitaifa.

Tabora. Mkuu wa shule kongwe ya Sekondari ya Tabora wavulana, Deogratias Mwambuzi, ametaja sababu kadhaa za shule yake kushika nafasi ya tano kitaifa, akisema ni mshikamano wa wafanyakazi, walimu na wanafunzi.

Akizungumzia matokeo ya shule yake yaliyotoka jana Alhamisi Julai 11, 2019, Mwambusi amesema walimu wamekuwa wakijituma na uongozi kutoa chakula kwao na fedha zinapopatikana kama motisha ili wajitume zaidi.

Amesema hata wanafunzi nao hupatiwa  motisha, jambo linalozidisha ushindani miongoni mwao.

Akizungumza na Mwananchi jana shuleni hapo, Mwalimu huyo amesema shule huwapatia majaribio mengi wanafunzi kwa lengo la kuwaimarisha na kuwafanya wasiogope mitihani.

Katika matokeo hayo mazuri, amebainisha kuwepo mwanafunzi Renatus Mgyabuso aliyepata alama tatu katika masomo ya PCM huku akijigamba kuwa wamejipanga mwakani kushika nafasi ya kwanza Kitaifa.

Shule hiyo ya wanafunzi wenye vipaji, imepata daraja la kwanza 87 na la pili wanafunzi 19 ikiwa haina madaraja mengine.