Takukuru inamshikilia mkandarasi wa miradi ya maji wilayani Nyasa

Kamanda wa Takukuru mkoani Ruvuma, Yustina Chagaka

Muktasari:

  • Mkandarasi wa mradi wa maji unaotekelezwa katika vijiji vitatu vya  wilaya ya Nyasa, anadaiwa kuingiziwa fedha za rushwa kwa awamu tatu kupitia akaunti yake ya benki

Songea. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa  mkoani Ruvuma (Takukuru) inamshikilia  Mhandisi wa maji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa, Evaristo Ngole kwa madai ya kushawishi  na kupokea rushwa ya Sh9 Milioni kutoka kwa mkandarasi.

Akizungumza na Mwananchi  ofisini kwake leo Jumatatu Juni 24, 2019, Kamanda wa Takukuru mkoani Ruvuma, Yustina Chagaka amedai kuwa mhandisi huyo aliomba fedha hizo kutoka kwa mkandarasi ili aweze kumpitishia  malipo yake ya kazi ambazo alikuwa amezifanya wilayani humo.

Amesema mkandarasi huyo alitekeleza mradi wa maji katika vijiji vya Lilondo, Asili na Lumecha na  kukamilika kwa wakati  kutokana na mkataba wake wa kazi, alidai wakati akisubiri kulipwa, ndipo mhandisi huyo alipofikia hatua ya kumshawishi kwa kumwomba kiasi hicho cha fedha na kumtaka akaziingize kwenye  akaunti yake iliyopo benki ya CRDB.

Kamanda huyo amesema mlalamikaji ambaye ndiye mkandarasi wa mradi huo unaotekelezwa katika vijiji hivyo wilayani, Nyasa, alidai aliingiza fedha hizo kwenye akaunti hiyo kwa awamu  tatu.

Na awamu ya tatu aliwekewa mtego na kufanikiwa kukamatwa baada ya fedha hiyo kuingia kwenye akaunti yake.

Kamanda   Yustina, amesema tatizo la rushwa linakwamisha miradi mingi ya maji mkoani Ruvuma.

Amesema Takukuru inatoa pongezi kwa makandarasi wote wanaozingatia weledi katika kutekeleza miradi ya maendeleo ili thamani ya fedha iweze kuonekana katika miradi hiyo na kuleta tija kwa Taifa.

Pia wanaendelea kuwaomba wananchi kuendelea kuunga mkono juhudi za mapambano dhidi ya rushwa kwa kukataa kujihusisha na vitendo vya rushwa  na kutoa taarifa za vitendo hivyo katika ofisi za Takukuru kusudi wahusika wachukuliwe hatua za kisheria.