Tanesco yatahadharisha wananchi wa Mtwara na Lindi

Muktasari:

Tanesco imewataka wananchi wa mikoa ya kusini kutokaa karibu na miundombinu ya umeme ili kuepuka madhara

Dar es Salaam. Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) limetaka wateja wake wa mikoa ya Lindi na Mtwara kuendelea kuchukua tahadhari ya uwezekano wa kuwepo kwa Kimbunga ikiwemo kutojikinga na mvua chini ya nguzo zilizobeba transfoma.

Taarifa iliyotolewa na Tanesco imeeleza kuwa wananchi wanatakiwa kuwa mbali na miundombinu ya umeme na kutokaa chini ya nguzo zote zenye nyaya.

“Iwapo utaona nguzo imeanguka ama waya kukatika toa taarifa Tanesco, usishike wala kukanyaga waya uliokatika,” taarifa hiyo imeeleza.

Tanesco imeshauri pia iwapo kimbunga kitaambatana na radi, upepo mkali au umeme kupungua nguvu na kuongezeka nyumbani,  wanatakiwa kuuzima kwenye kifaa cha ‘main switch’.

Taarifa za uwezekano wa kuwepo kimbunga kilichopewa jina Keneth mikoa ya kusini zinaendelea kutolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania.