Utouh: Tanzania ilianza kuharibika tangu nikiwa CAG
Muktasari:
- Ludovick Utouh, aliyekuwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) nchini Tanzania amesema nchi hiyo ilianza kuharibika tangu alipokuwa na wadhifa huo.
Dar es Salaam. Aliyekuwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Utouh amesema Tanzania ilianza kuharibika tangu alipokuwa akishika wadhifa huo, hasa ulivyokuwa utaratibu wa kulipana posho.
Utouh ambaye kwa sasa ni mkurugenzi wa taasisi ya Wajibu ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Desemba 7, 2018 jijini Dar es Salaam katika kongamano la maadhimisho ya miaka 70 ya haki za binadamu.
Utouh alistaafu kwa mujibu wa Sheria za Utumishi wa Umma baada ya kutumikia nafasi hiyo kwa miaka minane kuanzia 2006 hadi 2014 nafasi yake ilipochukuliwa na Profesa Mussa Assad.
Katika maelezo yake Utouh amesema katika uongozi wake watu walikuwa wakisafiri na kulipana posho hovyo huku wanaowasimamia wakiwa hawajali lolote.
Utouh aligusia sakata la uchotwaji wa mabilioni katika Akaunti ya Tegeta Escrow, akibainisha kuwa mamlaka zilieleza kuwa fedha hizo si za umma, kushangazwa jinsi watu wanavyosota rumande kwa ajili ya Escrow.
Ameipongeza Serikali ya Awamu ya Awamu ya Tano kwa kurejesha nidhamu na kuyafanyia kazi baadhi ya mapendekezo yaliyokuwa yakitolewa enzi za uongozi wake.
“Walau kwa sasa unaweza kusema kuna afadhali na ilivyokuwa hapo nyuma ambako hali ilikuwa ni mbaya sana. Kulikiwa na matumizi ya fedha ya ajabu, Serikali hii walau inathubutu kupunguza hizo tabia," amesema.
Otouh aligusia mapato na matumizi, ametahadharisha kuhusu utaratibu wa Serikali ya Awamu ya Tano kukusanya mapato yasiyoendana na utaratibu mzuri wa matumizi huku kukiwa hakuna mzunguko wa fedha jambo alilodai kuwa ni hatari katika uchumi.