Tanzania yashauriwa jinsi ya kukusanya mbegu

Muktasari:

Tanzania yashauriwa kuwa na mpango wa kitaifa wa ukusanyaji mbegu za mimea na miti utakaohusisha utafiti wa kina wa mbegu hizo kabla ya kuzihifadhi au kuanza kuzitumia

Mbeya. Mratibu wa taasisi ya Royal Botabic Gardens Kew kwa nchi za Afrika, Timothy Pearce ameishauri Tanzania kuwa na Programu ya kitaifa ya ukusanyaji wa mbegu za mimea yote ya porini.

Amesema hilo litarahisisha kazi ya ukusanyaji na kuondoa uwezekano wa taasisi tofauti kufanya kazi zinazofanana kama ilivyo sasa.

Pearce ameyasema hayo  jijini Mbeya jana Jumanne Juni 11, 2019 alipokutana na wataalam wa mbegu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kabla ya kuanza kukusanya mbegu za mimea midogo pembezoni mwa milima.

Alieleza ukusanyaji huo ni vyema ukahusisha aina zote za mimea kama  mizizi, vichaka na miti ya porini.

Alisema pamoja na kukusanya pia ameshauri mbegu hizo zifanyiwe tafiti kisha zipelekwe kwenye matumizi ikiwemo kuzipanda kwenye maeneo ya hifadhi yaliyoathiriwa.

Kaimu Meneja wa sehemu ya bailojia ya mbegu katika Kurugenzi ya mbegu TFS, Fandey Mashimba alisema wamepokea ushauri na wataufanyia kazi.

“Kitaalam jambo alilolisema lina tija na wataalam tumelielewa ndio maana nasema tumelichukua na tutalifanyia kazi, ukusanyaji huu umekuwa ukifanywa na taasisi nne tofauti,

“Ila kulingana na hawa wenzetu wataalam kuna uwezekano wa taasisi hizi kuungana na kufanya kazi hii kwa umoja zaidi,”

Alisema mratibu huyo na maofisa watendaji wa juu wa  Kew wamekuja nchini kushiriki kwenye ukusanyaji wa sampuli za mbegu za mimea midogo.

Mashimbe alieleza Tanzania inatarajia kujifunza vitu vingi kutoka kwa wataalam hao ambao wamebobea katika taaluma ya ukusanyaji mbegu na uhifadhi.