Tutarajie Facebook katika lugha za asili za Kitanzania

Muktasari:

  • Mtandao wa Facebook unafikiria kuanzia lugha za kiasili ili za Kiafrika  ili kuwavutia watumiaji wengi zaidi.

Dar es Salaam. Pengine siku moja tutashuhudia mtandao wa Facebook ukiwa katika lugha ya Kisukuma, Kinyanyusa au lugha yoyote ya asili, binafsi sipati picha itakuwa vipi huko mtandano, ila lugha ya kwanza kuingizwa wenyewe watatamba sana.

Uwezekano wa hilo kutokea unatokana na nia ya mtandao wa Facebook ambao una watumiaji hai zaidi ya bilioni 2.3 duniani kote kueleza nia yake ya kuendelea  kuongeza lugha za asili za Kiafrika katika mtandao huo.

Jumatano Agosti 14,2019 mtandao huo ulisema lugha kadhaa za asili zitaongezwa katika mpango wake wa kutathimini uhakika wa maudhui ‘Third-Party Fact-Checking programme’ ili kusaidia watumiaji kupata taarifa kwa usahihi kupitia mtandao huo na kuzuia usambazaji wa taarifa potofu.

Mpango huo tayari unahusisha lugha za Kiyoruba, Kiigbo na Kihausa kwa upande wa Nigeria, Kiswahili, Kesnya, Kiwolof Senegali na lugha za asili sita za Afrika Kusini kikiwemo Kizulu na Kisetswana.

Mkuu wa sera za facebook Afrika, Kojo Boakye alisema mtandao huo unaendelea kuwekeza katika jitihada za kuzuia usambazaji wa taarifa za uongo kupitia jukwaa la mtandao huo lakini pia kujenga jamii ya pamoja iliyo salama na yenye taarifa.

“Kwa kuongeza wigo wa lugha za asili kutaongeza ubora wa taarifa zinazoonwa na watu katika mdandao wetu, tunafahamu bado tuna mengi ya kufanya na tuko tayari kufanya,” alisema Boakye.

Aidha katika mpango huo, Facebook unashirikiana na taasisi inayojihusisha na kusimamia ukweli wa taarifa ndani ya Bara la Afrika (Africa Check) kwa lengo la kuangalia ukweli wa maudhui yanayowekwa katika mtandao huo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Africa Check, Noko Makgato alisema mpango huo kwao ni jambo jema kwakuwa wamepanua ghala la lugha. “Kwenye nchi za kiisimu kama Nigeria, Kenya, Afrika Kusini na Senegali kuangalia usahihi wa maudhui ni jambo muhimu,” anasema Makgato.