Uingereza yasema ATCL kufanya safari zake nchini humo ni fursa ya kiuchumi

Mwakilishi wa ujumbe maalum wa Waziri Mkuu wa Uingereza, Andrew Rosindell akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, baada ya mazungumzo ya awali ya ushirikiano kati ya shirika la ndege Tanzania (ATCL) na nchi hiyo, ikiwa ni mkakati wa shirika hilo kuanzisha safari ya kwenda uingereza. Kulia ni Mkurugenzi wa biashara wa ATCL, Patrick Ndekana. Picha na Ericky Boniphace

Muktasari:

Serikali ya Uingereza imesema  Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kuanzisha safari za ndege kutoka nchini humo kwenda Uingereza ni fursa ya kiuchumi kwa nchi hizo mbili

Dar es Salaam. Serikali ya Uingereza imesema  Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kuanzisha safari za ndege kutoka nchini humo kwenda Uingereza ni fursa ya kiuchumi kwa nchi hizo mbili.

Hivi Karibuni mkurugenzi mkuu wa ATCL, Ladislaus Matindi amesema mwishoni mwa mwaka 2020  shirika hilo litaanza safari zake kati ya Dar es Salaam, Tanzania na London, Uingereza na tayari limepata ratiba ya uwanja wa Gatwich.

Leo Jumatano Agosti 7, 2019 shirika hilo limepata ujumbe wa waziri mkuu wa Uingereza ukiongozwa na kiongozi wa kamati ya mambo ya nje, Andrew Rosindell ambaye amesema Tanzania ina mambo mengi ya kuipa Uingereza kupitia safari hizo.

"Kuna fursa kubwa ya kushirikiana katika kukuza biashara na uwekezaji kama utalii kupitia ndege ya moja kwa moja.”

“Kupitia safari hizo tutaimarisha urafiki wetu na mahusiano ya muda mrefu,  nina imani jambo hili litakuwa la manufaa kwa pande zote," amesema Rosindell aliyeambatana na balozi wa Uingereza nchini Tanzania,  Sarah Cooke.

Amesema lengo la ujumbe huo ni kusikia mipango, kueleza fursa, kushauri na kusaidia kufanikisha.

Mkurugenzi wa biashara wa ATCL,  Patrick Ndekana ameishukuru Serikali ya Uingereza kwa kuwaeleza fursa na nia ya kulisaidia shirika hilo kutimiza mipango yake, ameahidi kushirikiana nao ili kufanikisha jambo hilo.

"ATCL imekuwa ikishiriki kutangaza fursa za biashara na utalii hapa nchini,  hivi sasa tunataka kukuza soko la Ulaya. Kibiashara Jiji la London litatuunganisha na nchi nyingine za Ulaya na Amerika," amesema Ndekana.