Wananchi wafurika kutambua miili ya ndugu zao ajali Songwe

Askari wa Jwtz wakishusha majeneza kwa ajili ya kuhifadjia miili ya marehemu

Muktasari:

  • Robert Mwakilemile amesema baba yake, Sunday amekufa katika ajali hiyo, kwamba jana alikwenda jijini Mbeya kuitembelea familia yake na alikutwa na mauti wakati akirejea Tunduma

Mbozi.  Wakazi wa Tunduma, Vwawa, Mlowo na Mbeya wanaendelea kumiminika chumba cha kuhifadhia maiti Hospitali ya Mkoa wa Songwe kutambua miili ya watu 19 waliokufa baada ya kupata ajali usiku wa kuamkia leo Ijumaa Februari 22, 2019.

Ajali hiyo imetokea eneo la Mlima Senjele wilayani Mbozi.

Robert Mwakilemile amesema baba yake, Sunday amekufa katika ajali hiyo alipokwenda Mbeya kuitembelea familia yake na alikutwa na mauti wakati akirejea Tunduma.

Kwa upande wake Hassan Mwashambwa amesema amemtambua shemeji yake, Joseph Mbwama aliyefariki katika ajali hiyo.

Leo asubuhi zoezi la kutambua miili lilikuwa likiendelea lakini ilipofika saa 4 asubuhi lilisitishwa kwa muda ili madaktari kuiandaa miili vizuri kwa ajili ya kuiweka katika majeneza yaliyonunuliwa na Serikali ya Mkoa wa Songwe.

Mkuu wa wilaya ya Mbozi, John Palingo amesema zoezi hilo linasitishwa kwa muda ili wataalamu waweze kuiweka vizuri miili hiyo iwe rahisi kutambuliwa.