Wanawake wawili wabakwa, wauawa

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tanga, Edward Bukombe

Tanga. Matukio yenye kufanana ya kuwabaka wanawake kisha kuwaua yaliyotokea ndani ya saa 72 wilaya za Pangani na jijini Tanga, yameipa polisi kazi ya ziada ya kuchunguza sababu zake.

Usiku wa kuamkia Desemba mosi, muuguzi wa zahanati ya Kikokwe, Leah Mtega (18) alikutwa amekufa baada ya kubakwa kisha kunyongwa na jana alfajiri mwili wa Fatma Bakari (40) ambaye ni mlinzi wa kampuni ya G1 Security, ulikutwa umetelekezwa vichakani vilivyopo Gongagonga jijini Tanga. Askari huyo alikufa kwa kupigwa na kitu chenye ncha kali kichwani baada ya kubakwa.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tanga, Edward Bukombe alisema wanachunguza sababu za mauaji hayo yanayofanyika baada ya kuwabaka wanawake.

“Matukio haya yametupa kazi ya ziada ya kuchunguza ni kwa nini vijana wanawabaka kisha kuwaua,” alisema. (Burhani Yakub)