Watatu wanaswa na dawa za sangoma

Muktasari:

  • Kabla ya waganga wawili wanaodaiwa kutokea nchi jilani ya Kenya walioletwa na Maginga (muibiwa) kutoa dawa lilitolewa tangazo kwa wananchi kuwataka waliohusika kujitokeza kabla ya madhara,hata hivyo hakuna aliyejitokeza na kuanza kuwanyesha watu zaidi ya 40 na nyingine kunawa.

Serengeti. Wakazi wa kijiji cha Matare wilaya ya Serengeti Mkoa wa Mara wamekumbwa na taharuki baada ya watu watatu kupoteza kumbukumbu baada ya kunywa dawa ya kienyeji katika zoezi la kubaini wezi wa fedha za bonanza.

Tukio hilo limetokea juni 23 mwaka huu ikiwa ni baada ya watu wasiojulikana kuiba  zaidi ya sh 1.5 za bonanza na mali nyingine katika vibanda vya Mohabe Maginga na Rhoda Samweli juni 19 majira ya usiku mwaka huu na tukio kuripotiwa kituo cha Polisi Mugumu.

Kabla ya waganga wawili wanaodaiwa kutokea nchi jilani ya Kenya walioletwa na Maginga (aliyibiwa) kutoa dawa lilitolewa tangazo kwa wananchi kuwataka waliohusika kujitokeza kabla ya madhara, hata hivyo hakuna aliyejitokeza na kuanza kuwanyesha watu zaidi ya 40 na nyingine kunawa.

“Hii ni mara ya tano naibiwa nikienda Polisi hakuna kinachoendelea, pamoja na kuwa mimi ni mlokole kipindi hiki niliamua kutumia hii njia ambayo inaharakisha uchunguzi, walionaswa ni watatu ambao ni  mlinzi wangu Nyagori Marwa(39)Jumanne Marwa(26)na Marwa Isame,” alisema.

Alisema  waganga waliondoka kwa maelekezo kuwa watakaonaswa watalazimika kulipa vitu vilivyoibiwa ambavyo ni zaidi ya sh 1.5 mil,na gharama za waganga ambazo hakuzitaja,” mmoja amepelekwa kwa waganga wa kienyeji, wawili wako kwao, nasubiri ndugu waje tuzungumze maana dawa si ya kuua bali watarudishwa kwenye hali ya kawaida,” alisema.

Mgosi Marwa dada yake na Nyagori alidai baada ya watu kunywa dawa mdogo wake alipoteza uwezo wa kuzungumza,  anatoka udelele na hawezi kuzungumza,” akitembea kidogo anaanguka, anaokota okota nyasi, sisi hatukujua kama alihusika na wizi maana yeye alikuwa mlinzi, tunashindwa tufanyeje,” alisema.

Roda Samwel mmoja wa walioibiwa alisema,” mimi nimeishaibiwa mara nne ikiwemo tukio la juzi ambalo walibomoa ukuta wa kibanda changu wakanywa maziwa yote kisha wakaingia kwenye bonanza, kitendo hiki kimewaumbua maana tunapopeleka polisi hakuna mrejesho wowote,” alisema.

Mkuu wa wilaya hiyo Nurdin Babu alisema tukio hilo linawastua,” nimeagiza polisi waende eneo la tukio wafuatilie ili kubaini ukweli wa tukio hilo,” alisema.

Kamanda wa Upelelezi wilaya ya Serengeti Alfredy Kyebe alisema walifanikiwa kuwapata waathirika wa dawa hizo wawili kati ya watatu na wanaendelea na uchunguzi wa kilichotokea na uvunjaji wa vibanda hivyo viwili.