Waziri Mwinyi awasilisha bajeti ya ulinzi ya Sh1.84 trilioni

Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Hussein Mwinyi akiwasilisha hotuba ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2019/2020 kwa mwaka wa fedha 2019/2020 bungeni jijini Dodoma leo. Picha na Ericky Boniphace

Muktasari:

Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussein Mwinyi leo Alhamisi amewasilisha bajeti ya wizara yake ya mwaka 2019/20 ya Sh1.84 trilioni na kuelezea utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2018.19 ya Sh1.91 trilioni.

Dodoma. Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussein Mwinyi amewasilisha bajeti ya wizara yake ya mwaka 2019/20 akiliomba Bunge la Tanzania kumuidhinishia Sh1.85 trilioni.

Akiwasilisha bajeti hiyo leo Alhamisi Mei 16, 2019 bungeni jijini Dodoma, Waziri Mwinyi amesema kati ya fedha hizo, Sh1.72 trilioni ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Sh128 bilioni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.

Bajeti hiyo ni pungufu ukilinganisha na ile aliyoiwasilisha Mei 14, mwaka 2018 ya Sh1.91 trilioni.

Akielezea mtiririko wa bajeti ya mwaka 2018/19, Waziri Mwinyi amesema kati ya Sh1.91 trilioni, Sh1.67 trilioni ilikuwa ya matumizi ya kawaida na Sh234 bilioni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.

Amesema hadi kufikia Aprili 2019, fedha iliyokuwa imetolewa ni Sh1.61 trilioni sawa na asilimia 84.28 ya bajeti.

Waziri Mwinyi amesema kati ya fedha hizo, Sh1.44 trilioni ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Sh164 bilioni ni kwa matumizi ya maendeleo.

Amesema fedha za matumizi ya kawaida Sh1.31 trilioni zimetumika kulipa mishahara na posho mbalimbali kwa maofisa, askari, vijana wa mujibu wa sheria na wa kujitolea.

Baada ya kuwasilisha mjadala unaendelea bungeni na leo jioni itahitimishwa na Bunge.