VIDEO: Zitto abainisha walichoazimia kamati kuu

Muktasari:

  • Kamati Kuu ya ACT- Wazalendo iliyokutana kwa siku mbili Dar es Salaam, yaazimia kuendelea kupigania tume huru ya uchaguzi na uchaguzi huru.
  • Yaazimia kuendelea kushirikiana na vyama vingine vya upinzani ili kupigia demokrasia.


Dar es Salaam. Kamati Kuu ya ACT -Wazalendo iliyoketi kwa siku mbili jijini Dar es Salaam imeazimia mambo mbalimbali ikiwemo kuimarisha ushirikiano na vyama vingine vya upinzani katika kutetea, kuipigania na kuilinda misingi ya demokrasia nchini Tanzania ambayo chama hicho kimedai imevurugwa.

Pamoja na hilo, chama hicho kimetoa salamu za mshikamano kwa wananchi wa Sudan ambao wanapitia katika kipindi kigumu cha kupigania demokrasia nchini kwao, hasa baada ya kufanikiwa kuangusha utawala wa Rais Omar Al Bashir.

Maazimio hayo yamesomwa leo Jumanne Juni 11, 2019 na Kiongozi wa ACT- Wazalendo Zitto Kabwe  kwa niaba ya wajumbe wa kamati Kuu ya chama hicho iliyoketi Juni 9 na 10, 2019 katika ofisi ndogo za chama hicho Magomeni Dar es Salaam.

Zitto ambaye pia mbunge wa Kigoma mjini amesema azimio jingine ni pamoja kamati kuendelea kushiriki kupigania Tume huru ya uchaguzi kwa kuwapongeza mwanaharakati Bob Chacha Wangwe na mwanasheria Fatma Karume aliyesimamia kesi ya kubatilisha vifungu kwenye sheria inayowapa vifungu wakurugenzi kusimamia uchaguzi.

"Kamati Kuu imewaagiza wanasheria wa chama kufungua kesi ya kikatiba chini Tanzania ya hati ya dharura kuomba tafsiri ya mahakama iwapo hukumu ya Mahakama Kuu kwenye kesi ya Wangwe inaathiri ushiriki wa wakurugenzi wa halmashauri kama wasimamizi kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa," amesema Zitto