Kwa waliokosea kutuma pesa, Jihudumie hii hapa

Mtendaji Mkuu kitengo cha Tigo pesa, Hussein Sayed.

Muktasari:

  • Akizungumza na wanahabari leo Alhamisi Julai 12, 2018 wakati wa uzinduzi wa kampeni ya Tigo Pesa ni Zaidi ya Pesa, Mtendaji Mkuu kitengo cha Tigo pesa, Hussein Sayed amesema huduma hiyo itamwezesha mteja kuzuia miamala yoyote ya kutuma fedha ikiwa watagundua kuwa wamekosea.

Dar es Salaam. Kampuni ya simu ya Tigo imeanzisha huduma ya kuzuia miamala iliyokosewa kwa kutuma fedha kwa mtu ambaye si mlengwa iliyopewa jina la “Jihudumie”.

Akizungumza na wanahabari leo Alhamisi Julai 12, 2018 wakati wa uzinduzi wa kampeni ya Tigo Pesa ni Zaidi ya Pesa, Mtendaji Mkuu kitengo cha Tigo pesa, Hussein Sayed amesema huduma hiyo itamwezesha mteja kuzuia miamala yoyote ya kutuma fedha ikiwa watagundua kuwa wamekosea.

“Sasa hivi mtu akikosea kutuma pesa hahitaji msaada wa moja kwa moja kutoka kitengo cha huduma kwa wateja bali atapiga atakwenda menyu ya Tigo pesa kisha mteja atachagua huduma ya Jihudumie,”amesema na kuongeza kuwa:

“Huduma hii haitatumiwa kwa wale ambao pesa imeshatumwa kimakosa na mpokeaji ameshaitoa hapo anatakiwa kufanya mawasiliano na kitengo cha huduma kwa wateja.”

Amesema huduma hiyo inawapa uwezo wateja juu ya miamala wanayofanya na imeundwa kwa kuzingatia vigezo vitakavyozuia matumizi mabaya ya huduma ya Tigo pesa.