MAONI: Dawa za kulevya na athari zake katika biashara

Muktasari:

Dawa za kulevya huchochea makosa mengi ya kijamii ukiwamo ushoga, ukabaji hata wizi na ujambazi. Mambo haya yote huwahusisha vijana ambao ni nguvukazi muhimu ya kujenga uchumi. Biashara na ujasiriamali ni sekta za kwanza kuathiriwa na matumizi ya dawa za kulevya.

Hivi karibuni Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alijaribu kupambana na watu wanaojihusisha na mapenzi ya jinsia moja. Vita alivyovianzisha vilizua mjadala kidogo kwa wadau kujitokeza na kusema linalowakereketa.

Licha ya ushoga, dawa za kulevya ni janga jingine linalohitaji mkakati kukabiliana nalo.

Kama ilivyokuwa maeneo mengine, ujasiriamali na biashara ndogo zinazojumuisha taasisi ndogo za fedha zinaathirika kutokana na lolote linaloendelea kwenye jamii inayojihusisha nayo kila siku kutokana na bidhaa au huduma zake.

Kutokana na ukweli kuwa watumiaji na waathirika wengi wa dawa za kulevya ni vijana wa rika la uzalishaji wenye nguvu za mwili na akili, ni vizuri kutambua kuwa dawa hizi zinaharibu rasilimali watu ambayo ingeweza kufanya kazi kwenye miradi tofauti na kuchangia kukuza uchumi.

Vijana hawa, kama hawatakuwa wamiliki wa biashara, basi wanaweza kufanya shughuli nyingine zitakazochangia kuimarisha na kuongeza mnyororo wa thamani ukapata fedha na faida nyingine za huduma.

Vilevile, taasisi ndogo za fedha zinawahitaji vijana wasomi kwa ajili ya uendeshaji, uongozi na ubunifu utakaofanikisha huduma zenye tija kwa wananchi na kukua kwa ofisi husika.

Dawa hizi zinafanya idadi yao kupungua kwenye soko la ajira, hivyo kuwafanya kuwa adimu kusimamia taasisi hizi pendwa na kupunguza au kupoteza nafasi ya kuwa na wataalamu wengi kwenye sekta muhimu ya fedha. Dawa za kulevya zinaua soko la bidhaa na huduma za wajasiriamali pamoja na taasisi ndogo za fedha kutokana na ukweli kuwa uwezo wa kununua bidhaa kwa watu wengi utakuwa unapungua kutokana na uwapo wa waathirika ambao hawana nguvu ya kufanya kazi.

Licha ya hivyo, kukosa kipato cha uhakika kutokana na kushindwa kufanya kazi kunawanyima nafasi na uwezo wa kununua bidhaa na huduma za wajasiriamali na itakayokuwa inawalea waathirika hawa kuanzia ngazi ya familia uwezo wao wa kiuchumi utapungua kutokana na gharama za kufanya hivyo.

Kwa sababu gharama za kuwalea vijana hawa ni kubwa kiasi cha kuyumbisha shughuli za wajasiriamali, athari hizo hufika mpaka kwenye taasisi ndogo za fedha ambazo hupata ugumu wa kufanya biashara na kundi la watu wa namna hii kwa sababu kufanya hivyo ni kuhatarisha fedha zao.

Kupungua na kupotea kwa usalama kwenye mazingira ya kufanyia kazi kwa wajasiriamali na taasisi ndogo za fedha, kutokana na kukua kwa kundi la waathirika wa dawa za kulevya hasa wenye kipato cha chini mara nyingi huwafanya wahusika wajiingize kwenye uhalifu wakati mwingine wa kutumia silaha ili kutafuta fedha za kuwawezesha kununua tena dawa hizo. Ikifikia hatua hii wajasiriamali wadogo pamoja na mali zao wanakuwa hatarini kuvamiwa na kuporwa au wakati mwingine kupoteza maisha kitu kinachodhohofisha ukuaji wa uchumi.

Suala hili pia huziathiri taasisi ndogo za fedha na kuziweka kwenye kwenye hatari ya kuvamiwa na kupoteza mtaji hivyo huleta hasara na kupoteza muelekeo wa watu wengi sana wanaonufaika na huduma zao. Pasipokuwa na amani na utulivu ni ngumu kutengeneza uchumi imara na wenye nguvu.

Kujihusisha na dawa za kulevya ni kosa kisheria hivyo ni vizuri taasisi na ofisi husika zikaendelea kupambana na tatizo hili bila kuchoka kwa ushirikiano na wadau wengine kwa kufuata utaratibu ili kuhakikisha vijana wanaacha kujihusisha nazo na kufikiria kufanya mambo tofauti yenye tija kwa jamii na taifa kwa ujumla.

Tufumbue macho na kuingia kwenye ujasiriamali, kila mtu kwa nafasi yake, ili kuitengeneza Tanzania ya viwanda.