Ali Ali, ana umbo dogo lakini mambo makubwa

Muktasari:

  • Simba ilitoka sare ya mabao 3-3 na Chama la Wana, wakati Yanga iliibuka na ushindi wa mabao 3-1, mechi zote zilichezwa Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam, beki huyo alikuwa mwiba kwa mastraika wa timu hizo.

Ukimuuliza John Bocco, Emmanuel Okwi (Simba), Obrey Chirwa na Ibrahim Ajib (Yanga), watakujuza shuguli ya beki wa Stand United ‘Chama la Wana’ Ali Ali ambaye alikuwa anavuruga mipango yao, walipokutana kwenye mechi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Simba ilitoka sare ya mabao 3-3 na Chama la Wana, wakati Yanga iliibuka na ushindi wa mabao 3-1, mechi zote zilichezwa Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam, beki huyo alikuwa mwiba kwa mastraika wa timu hizo.

Spoti Mikiki imefanya mahojiano na Ali Ali ambaye amezungumzia safari yake ya soka na ndoto zake za badae katika soka, ilikuwa kama ifuatavyo.

Ali Ali anasema alikuwa anacheza soka kama kujifurahisha na hakujijua kama ana kipaji, mpaka makocha walipomwambia aelekeze nguvu katika kazi hiyo na kwamba atafika mbali.

“Akili ya utoto ilikuwa ya ajabu, nilikuwa si mpenzi sana na shule, wala nilikuwa sitilii manani sana soka, mpaka nilipokuja kuambiwa na meneja wangu anayeitwa Kamali Manji kwamba nina kipaji natakiwa kuzingatia mazoezi, alikuwa makini kuninunulia vifaa vya michezo,”anasema.

Akizungumzia ratiba yake kwa siku anasema anaanza na mazoezi, akimaliza anaoga na kupumzika, ifikapo mchana anapata chakula kidogo kinachokuwa kimepatikana kwa wakati huo, lakini matunda na maji anatumia kwa wingi.

“Sio mpenzi wa kunywa chai asubuhi, mchana nakula kidogo sana ila kwa usiku unakuwa ni mlo wa kutosha na maji mengi kwa wastani namaliza katoni tatu kwa usiku tu,” anasema.

Ali aliyeanzia soka yake Mkunazini ya Zanzibar 2012, pia alichezea Vikokotoni ya Daraja la pili 2014 na kuhamia Gulioni kati ya 2015-16 na Stand United mwaka 2017-18.

Ndoto yake anasema kabla ya kupata nafasi ya kucheza nje, anatamani apitie timu moja wapo kati ya Azam, Simba au Yanga.