Ana kiuno kizito hadi najiuliza somo yake nani?

Muktasari:

  • Pole sana. Hujasema una muda gani naye kiasi cha kuchoka kumfundisha kukata nyonga. Ila nina wasiwasi na wewe ni mzito ndiyo maana inamuwia vigumu kukuonyesha ujuzi wake.

Anti habari! Natamani nikuletee mamsapu wangu umtafutie wataalamu wamfundishe kunyonga, ana nyonga nzito nimejitahidi kumfundisha namna ya kukinyonga nimeshindwa.

Najiuliza kama somo yake alifanya kazi yake wakati wa kumuandaa ili awe mke wangu.

Nifanyeje?

Pole sana. Hujasema una muda gani naye kiasi cha kuchoka kumfundisha kukata nyonga. Ila nina wasiwasi na wewe ni mzito ndiyo maana inamuwia vigumu kukuonyesha ujuzi wake.

Kabla hujampeleka kwa wataalamu mueleze jinsi unavyopenda mwanamke anayezungusha nyonga kisawasawa, kwa sababu wapo wanaume wasiopenda mambo hayo, hivyo anaweza kudhani na wewe ni miongoni mwao.

Jitahidi unapokuwa kwenye mazungumzo ya mahaba uwe na unamweleza unavyotamani na yeye ajue kujikunja kunja kama nyoka muwapo faragha, hiyo itamuingia akilini na ataanza kufanya mazoezi akiwa peke yake.

Ananionea wivu hadi nakosa raha

Habari za kazi, pole na majukumu. Naomba ushauri labda utanisaidia kuwa na amani, mke wangu amezidi kunionea wivu hadi nakosa raha.

Nikiwa kazini anasema nipo na wanawake zangu, nikiwa na washikaji anasema wananitafutia wanawake, nikienda mpirani anasema nimekwenda kutafuta wanawake, hataki hata niimbe nyimbo zenye majina ya kike anasema ninawataja wanawake zangu kijanja.

Nifanyeje?

Hilo donda umelilea tangu likiwa changa sasa limekuwa dinda ndugu linakunukia mwenyewe, mwanamke ana wivu wa aina hiyo na bado hujachukua hatua za kuhakikisha unaukomesha.

Usiruhusu hali hiyo kwenye familia yako utakosa raha, hutakuwa na marafiki na atakufanya ujione mkosaji kila siku.

Kuanzia leo akikueleza kuwa upo na wanawake zao mjibu ndiyo, acha kujitetea kwa vitu ambavyo hujafanya, kama umeshatumia muda mwingi kumuelewesha haelewi ipo siku atawatukana watu unaofanya nao kazi ukiendelea kumlea.

Mueleze kabisa kuanzia sasa hutaki kusikia wivu usiokuwa na sababu. Akitaka akufuatilie ili aone hicho anachokifikiria. Kemea hii tabia kama unaamini anakushutumu kwa mambo usiyoyafanya.

Ndoa ni furaha katika maisha na ni faraja kwa familia, kwa maisha hayo mnayoishi hizi maana zote zitapotea, atakufarakanisha na watu. Usiruhusu hali hiyo.