Bashe: Hata mimi naweza kuhama CCM kama hakitakuwa na tija kwa wananchi

Mbunge wa Nzega, Hussein Bashe akizungumza katika mkutano wa kampeni za mgombea Ubunge wa Jimbo la Ukonga kwa tiketi ya CCM, Mwita Waitara uliofanyika kwenye Viwanja vya Mwanagati Kitunda, jijini Dar es Salaam juzi. Picha na Said Khamis

Muktasari:

  • Kwa mujibu wa Bashe, hata yeye anaweza kuhama endapo chama chake cha CCM hakitakuwa na tija kwa wananchi.

Dar es Salaam. Mbunge wa Nzega Mjini, Hussein Bashe amesema zipo sababu za kwa nini aliyekuwa mbunge wa Jimbo la Ukonga (Chadema), Mwita Waitara kuhama chama hicho na kujiunga CCM kwa kuwa ni haki ya kisheria.

Kwa mujibu wa Bashe, hata yeye anaweza kuhama endapo chama chake cha CCM hakitakuwa na tija kwa wananchi.

Bashe ambaye alikuwa akizungumza katika kampeni za kumnadi mgombea huyo wa ubunge Jimbo la Ukonga kupitia CCM alisema ipo hoja inayosemwa kwamba Waitara amenunuliwa, hilo si kweli na kwamba anamfahamu kiongozi huyo tangu wakiwa pamoja Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM).

“Mwanasiasa yoyote anapoamua kuwatumikia wananchi anapanda basi, vyama vya siasa ni sawa na basi, ukiona basi hilo dereva, kondakta hamuelewani unaweza kushuka kwenye basi hilo,” alisisitiza Bashe.

“Aliondoka mzee (Augustine) Mrema mwaka 1995, Maalim Seif naye akaondola hadi mzee wangu (Edward)Lowassa alifanya hivyo, hatujawahi kutuhumu kama mtu amenunuliwa,” alisisitiza.

Kwa mujibu wa Bashe, hiyo ni hoja dhaifu inayotolewa na wanasiasa walioshindwa kufikiri; “wanaosema tulimnunua Waitara wao watuambie walimnunua kwa shilinga ngapi mwaka 2008,” aliongeza.

“Hakuna jambo linanisikitisha mimi kama kijana eti kwamba mwanasiasa anapohama chama anatuhumiwa amenunuliwa. Hata sisi wana CCM chama chetu kinaposhindwa kusimamia masilahi, au kutatua matatizo ya watu ukiona mimi nimebaki CCM jua tunalinda matumbo yetu,” alisema.

Mbunge huyo amevitaka vyama vya upinzani nchini kujitathmini ndani ya vyama vyao na kuacha kuituhumu CCM kwamba inanunua wabunge na madiwani wao.

Kutokana na tuhuma kwamba CCM imepanga kumteka mgombea wa Chadema, Asia Msangi, Bashe alivitaka vyombo vya ulinzi na usalama vimpe ulinzi wa kutosha mbunge huyo.

“Naviomba Vyombo vya ulinzi na usalama vimpe ulinzi, tulipuuza puuza maneno yakatokea maafa uchaguzi wa Kinondoni. Kama wanasema mgombea wao atatekwa wamuwekee ulinzi nyumbani kwenye gari na kila sehemu,” alisema Bashe.

Kuhusu gharama za uchaguzi kuwa kubwa kutokana na kurudiwa, Bashe alisema hakuna jambo lisilokuwa na gharama hata kwenda peponi kwa Mungu kuna gharama lazima usali, utoe sadaka, utoe zake na lazima ufe.

“Wanasiasa wanaosema chaguzi ndogo ni gharama leteni muswada bungeni tubadilishe sheria ili mtu akihama ahame na ubunge wake,” alisisitiza.

Awali mwenyekiti wa CCM Kata ya Tandale, Tamim Omari Tamim alisema vyama vya upinzani vimekufa ndiyo maana wanachama wake wanahamia chama hicho tawala.

“Vyama vya upinzani vimekufa. Ukisia CUF, sijui Chadema na wewe ukaingia kichwa kichwa basi akili huna,” alisisitiza mwenyekiti huyo.

Alisema wananchi wakimchagua Waitara atakuwa mkombozi wao kwa kuwa wakazi wengi ni kabila lake hivyo hawezi kuwaangusha.

“Nimesikia eti hapa kuna wapinzani, mimi nataka niwambie kama kulikiwa na mpinzani mkubwa kwenye nchi hii basi nikuwa mimi. Nilikuwa CUF tangu 1992 kabla ya Katibu Mkuu wa chama hicho taifa Maalim Seif Hamad na Mwenyekiti Profesa Ibrahim Lipumba,” aliongeza.

Kwa upande wake mbunge wa Mtera, Livinstone Lusinde alisema mawaziri wakuu wastaafu Frederick Sumaye na Edward Lowassa baada ya kujiunga na vyama vya upinzani wamekuwa wanafiki kwa kuwa wanayo yaahidi hawawezi kutekeleza.

“Suala la kuja CCM sio suala la dharura..Kinachowasumbua ni kwamba wanafahamu nguvu zangu ni kubwa sana ni jeshi la mtu mmoja.”