Nani ni nani kati ya China na Afrika?

Muktasari:

  • Miradi mikubwa Kiwanda cha Urafiki pamoja na reli ya Tazara ni moja ya miradi mikubwa iliyofanywa na serikali ya China barani Afrika.

Tangu miaka ya 1960 China imekuwa ikiwekeza kwa wingi barani Afrika hususan kwenye miundombinu ya barabara, reli na majengo. Zipo kampuni nyingi za kichina barani Afrika, ikiwamo Tanzania, ambazo zimewekeza na kufanya shughuli zake nchini katika uwekezaji huo.

Miradi mikubwa Kiwanda cha Urafiki pamoja na reli ya Tazara ni moja ya miradi mikubwa iliyofanywa na serikali ya China barani Afrika.

Taarifa kutoka katika kituo cha utafiti wa masuala ya uhusiano wa China na Afrika kipo katika Chuo Kikuu cha Hopkins, Marekani zinasema kuwa kipindi cha mwaka 2000 hadi 2016 China imewekeza kiasi cha zaidi ya Dola125 bilioni katika bara la Afrika.

Hata hivyo, katika mkutano uliofanyika mapema wiki hii, China imesema itaendelea kuisaidia Afrika katika ujenzi wa miundombinu pamoja na masuala ya ulinzi na kiusalama.

Serikali ya China ilifadhili mradi wa ujenzi wa reli kutoka Nairobi mpaka bandari ya Mombasa nchini Kenya uliogharimu kiasi dola 3.2 bilioni. Mradi wa reli hiyo iliyotegemewa kuunganisha nchi za Rwanda, Burundi, Sudan Kusini na Ethiopia, umeonekana kusuasua baada ya kubainika kutia hasara ya zaidi ya Dola100 bilioni katika kipindi cha mwaka mmoja tangu kukamilika kwake.

Mkutano uliofanyika Beijing, wiki iliyopita Serikali ya China ilisema itatoa Dola60 bilioni ifikapo mwisho wa mwaka huu.

Ndoa ya China na Afrika

Rais wa nchi hiyo, Xi Jinping alisema China haiwekezi katika miradi isiyo na maana, bali inalenga kulisaidia bara la Afrika kujenga miundombinu na kuifanya nchi hiyo kuwa pekee inayowekeza kiasi kikubwa cha fedha barani Afrika.

Pamoja na hayo, wakosoaji wameonya kwamba mataifa ya Afrika yamejikuta yakiingia katika madeni isiyoweza kumudu kutoka kwa nchi hiyo kubwa barani Asia. Akifungua mkutano huo wa siku mbili, Rais Jinping aliwaambia viongozi na wafanyabiashara kutoka Afrika kuwa ushirikiano wa China na bara hilo umelenga kuiletea Afrika maendeleo.

“Rasilimali zinazotokana na ushirika wetu hazipaswi kutumika katika miradi hewa bali katika miradi inayoonekana na yenye tija kubwa,” alidokeza.

Msomamo huo uliungwa mkono huku Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa akieleza wazi kuwa hakubaliani na wale wanaotaka kuwaaminisha kwamba hii ni aina mpya ya ukoloni inayotaka kulikumba bara la Afrika. Mataifa yote ya Afrika yalikuwa na uwakilishi katika mkutano huo isipokuwa Swaziland ambayo ina ushirika na Taiwan. Wakati huohuo China inadai Taiwan ni sehemu ya nchi yake, hivyo kufungamana na Taiwan ni kama kuisaliti China, hivyo Swaziland isingeweza kuwa na ushirika na China na Taiwan kwa wakati mmoja.

Licha ya ukosoaji mkubwa unaelekezwa katika ushirika huo, Rais Jinping aliendelea kusisitiza kuwa uhusiano huu hauna mahusiano yoyote ya kisiasa bali ni nia ya dhati kabisa ya kuisaidia Afrika katika ujenzi wa miundombinu yake bila masharti yoyote.

Kiasi hicho cha fedha kitakuwa kama mkopo na msaada ikijumuisha ujenzi wa miundombinu na ufadhili wa masomo.

Kwa hakika ushirikiano huu umeonekana msaada mkubwa kwa Afrika ukilinganisha na vile ambavyo hali ingekuwa bila msaada wa China.

Hata hivyo, katika hili kuna mambo ya kutazama kwa kina kabla hujashangilia au kuukosoa ushirikiano na makubaliano haya. Ili uweze kufanya hivyo haupaswi kuwa upande wowote.

Wakosoaji wengi wamekosoa kwa kuwa pengine watakosa fursa za mataifa yao kuwekeza barani Afrika au pengine wamekwishaathirika kwa kiwango kikubwa na madeni haya au kinyume chake.

Lakini, ukikaa nje ya makubaliano haya na utazame kama hakimu asiyemfahamu mtu yeyote katika kesi, kisha usikilize maelezo ya pande zote mbili kwa weledi, upokee ushahidi halafu utoe maamuzi utaweza kutoa maamuzi sahihi.

Hata hivyo, hii sio kesi ya kuamua ni jambo ambalo linakupasa utazame hali halisi ya Afrika na China halafu uone ni yupi ananufaika zaidi, hasa kwa kuwa kimsingi pande zote zinanufaika.

Ni kweli usiopingika kuwa kwa kipindi kirefu China imeisaidia Afrika kwa mikopo na misaada mbalimbali, lakini katika hili sioni nchi kama China iliyo tayari kuwekeza kwa hasara, ninaiona China ikipanda punje moja ya mhindi kisha ivune punje nyingine hamsini.

Kama ni kweli China imekuwa ikitoa fedha kwa ajili ya kuiendeleza Afrika, ni vipi nchi hizi zimeshindwa kuendelea huku yenyewe ikizidi kunawiri katika uchumi wake?

Hivi majuzi bidhaa za China zimeongezewa kodi nchini Marekani, China nayo ikajibu kwa kuongeza kodi katika bidhaa za Marekani nchini mwake. Ulaya nako hakueleweki ndio kwanza (Waziri Mkuu) Theresa May wa Uingereza na (Kansela) Angela Merkel wa Ujerumani wanapishana angani. Unafikiri China itauza wapi bidhaa zake, unafikiri ataungwa mkono na nani kama si Afrika? Kwa hali hii China haiwezi kupoteza fedha na rasilimali zake bure. Katika hili fikiria vyema kisha jijibu bila kupepesa macho.

Keti chini kisha tulia halafu tazama vyema utaona nchi mbili kubwa (China na Marekani) zikikimbizana katika chati ya nchi zenye uchumi mkubwa duniani, kisha geuka tazama mzozo wa kibiashara unaoendelea kati ya nchi hizo mbili. Baada ya kutazama kwa makini utapata jibu lako, lakini mimi nikitazama sioni kama kuna nchini yoyote kati ya hizi (China na Marekani) inataka kushindwa kirahisi, sioni kama kuna nchi iliyo tayari kupoteza ubabe wake kiuchumi kwa kutapanya fedha na kupoteza muda zaidi, bali itataka kujiimarisha. Vilevile sioni kama kuna nchi iliyoko tayari kusinzia ipigwe kikumbo.

Baada ya kutazama uwekezaji wa China kwa Afrika, ninageuka upande mwingine na kuiona Afrika isiyo na teknolojia na miundombinu ya kutosha na kuiona China kama msaada mkubwa.

Ukiachilia mbali reli ya Nairobi kwenda Mombasa, barabara, madaraja, viwanda na viwanja vya ndege vilivyopo katika nchi mbalimbali ikiwemo Tanzania, ninawatazama wanafunzi wengi kutoka Afrika wakipewa ufadhili kwenda kusoma China katika fani mbalimbali ikiwemo uhandisi na afya, ninakiri kwamba kama sio China haya yasingekuwepo. Lakini, inakuwa vigumu kuamini kama wanafanya haya bila ya wao kupata faida yoyote.

Nazifikiria fursa za kibiashara, kiafya na kielimu zilizopo baina ya China na Afrika ninaona kwa kiasi fulani China imetutoa mahala ambapo tulikuwa na kutuweka mahala tulipo kwa sasa. Ninatazama miundombinu ya usafiri iliyopo katika majiji mbalimbali, ninaiona kama mkombozi kwa kiwango chake. Hata hivyo, ni vipi China inaweza kufanya yote haya bila yenyewe kufaidika?

Soko la bidhaa za China

Soko la bidhaa za China, ni mara kadhaa tumekuwa tukisikia malalamiko kwamba bidhaa za nchi hiyo hazina ubora bila, zipo bidhaa zinazokuja kulingana na thamani ya soko lililopo.

Kwa sasa China inaitazama Afrika kama mnunuzi mkubwa wa bidhaa zake. Inakuja kama mwekezaji ili kufungua milango ya bidhaa zake kuuzwa kwa wingi Afrika. China inatupatia mikopo kisha itaingiza bidhaa zake na kuvuna fedha, itakusanya mikopo yake na kuondoka sisi tukifurahia barabara na reli ambazo uendeshaji wake unatugharimu kiasi kikubwa cha fedha.

Mwandishi ni Mwanafunzi wa Shahada ya awali ya Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Anafanya mazoezi kwa vitendo Mwananchi Communications Ltd.

0762395558