Roma Mkatoliki amerudi tena

Ibrahim Musa maarufu Roma Mkatoliki amerudi tena na tungo zilizoamsha hisia za mashabiki wa muziki na kuwa gumzo mitandaoni.

Wimbo mpya wa msanii huyo unaitwa ‘Anaitwa Roma’.

Wimbo huo aliouachia kwenye mtandao wa YouTube ukiwa ni saa 18 tangu uwekwe ulikuwa umesikilizwa na watu 174,000 .

Wimbo huo amemshirikisha msanii One Six umekuwa gumzo kwenye mitandao huku watu wakihofia unaweza kumtia matatani wakihusisha na tukio la kutekwa kwake la mwaka 2017.

Aprili 7, 2017 msanii huyo akiwa na wenzake watatu walichukuliwa na watu wasiojulikana wakiwa kwenye studio ya Tongwe Records iliyopo Masaki Dar es Salaam wakifanya kazi ya kurekodi nyimbo.

Msanii huyo na wenzake walikaa mikononi mwa watu hao kuanzia siku ya Jumatano na kuachiwa Ijumaa.

Tukio hilo lilihusishwa na aina ya nyimbo anazoimba na ndiyo maana alipotoa wimbo huu umezua mjadala.

Watu wengi waliokuwa wakiujadili walikuwa wanamsifia na kumuonya kwa pamoja.

Kwenye mtandao wa Instagram waliousikiliza wimbo huo walisema:

onkolonkonchwa: kwani mzee haujaitwa basataa wanakusubiri ujee ila hongeraa ni bonge la ngomaa…

streetboyz509: Roma utekwi tena mzee bb ushaaga UK huko…

emanuelmadale7: ngoma kali kichiz sema nawaza sjui kama imepita Basata.

abelianpaul: Oyaa tulia kwanza huko Marekani waxije wakakuteka tena

tuwabin: Huyuuuu ndo romaa tunaye mjuwaa.

otanaely: Roma hizo tungo kali la waraka wa waebrania

noshadymangule: Nimeshaipakua brother goma lipo sawa kbs yn ni Dua brother

namungofcsupporters: Mnapiga Bomu Monchwari alafu mnajisifu mmeua

kassumbi: Safari hii wakikukamata kaka haurudi kabisa angalia wahuni sio watu wazuri aisee…

ozil_mattarjr: hii nyimbo imenigusa sana nyimbo imegusa maisha yetu halisi…

the_ceo: Hivi huyu jamaaa kaenda Marekani kaenda nafamilia yake au...

skak_wiz_tz: Tuwekee namba kaka tuanze kabisa kuchanga hela ya dhamana..

Roma mwenyewe alipowasiliana na Mwananchi kujua alilenga nini kutunga mashairi hayo na anachukuliaje onyo analopewa na mashabiki wake licha ya kupongezwa pia alijibu kwa kifupi.

“Nitakujibu sipo sehemu rafiki kwa mazungumzo hayo, ” alijibu Roma.