Shabiki anena, Kiba hata akiimba mabata madogo nitampenda tu

Shabiki wa msanii Ali Kiba, anayejulikana kwa jina la Emiliana Mgema, amesema anampenda msanii huyo ambaye anaamini nyimbo yoyote anayoimba ni nzuri kwake.

Emiliana alionyesha ushabiki wake kwa msanii huyo Desemba 22 mwaka huu wakati wa tamasha la fiesta lililofanyika viwanja vya Posta, ambapo alijikuta akilia mwanzo hadi mwisho Kiba alipopanda jukwaani kuimba.

Alipoulizwa kuhusu kilio hicho, Emiliana ambaye ana miaka 23, anasema imetokana na namna anavyompenda Kiba maarufu kama King Kiba na kushindwa kuzuia hisia zake. “Mimi Kiba namzimikia sana hata aimbe wimbo wa mabata madogomadogo nitapenda tu naomba aelewe hilo, ”anabainisha Emiliana ambaye anafanya biashara ndogondogo.

Tayari Ali Kiba ametangaza kumpa ofa ya tiketi dada huyo katika shoo yake ya ‘Funga mwaka na KingKiba’ itakayofanyika leo katika klabu ya Next Door Arena Masaki ambapo pia ameahidi kumpa kinywaji cha mofaya za kutosha.

“Shoo itaanza saa moja usiku lakini mimi nitafika eneo hilo saa nne asubuhi, ”amesema Emiliana.