Anakomaa na ubuyu wa embe mpaka umtoe

Muktasari:

  • Maisha yanataka uvumilivu kwenye kila unachokifanya. Mary anatuonyesha hilo kwenye biashara yake ya ubuyu wa embe. Wewe unakomaa na nini?

Mara nyingi tumezoea kuona embe zikitumika katika kutengeneza juisi au siki, lakini sasa matumizi yameongezeka ikiwamo kutumika katika kutengeneza ubuyu.

Ubuyu utokanao na embe unaelezwa kuwa na ladha nzuri zaidi na kufanya watu wengi kuvutiwa nao.

Marry Lazaro (29) ambaye ni mhitimu wa shahada ya ununuzi na ugavi katika Chuo cha Uhasibu, aliamua kuitumia fursa ya uwepo wa embe kujiingizia kipato ikiwa ni baada ya kukaa kwa muda mrefu bila ya ajira.

“Nilikuwa na mtaji wa Sh30,000 ambapo nilinunua ubuyu na kupata faida ya Sh15,000 ambayo ilitumika tena kukuza mtaji ambao sasa unakaribia kufika Sh700,000,” anasema Marry.

Anasema pakiti moja ya ubuyu huo huiuza kwa Sh30,000 huku soko lake kubwa akilipata kupitia mitandao ya kijamii ingawa wakati mwingine amekuwa akishindwa kuwafikia wateja wake kutokana na umbali “wengine wanaoagiza ubuyu wako maeneo ambayo ni ngumu kufikika kwa urahisi, kadiri unavyotangaza ndivyo idadi ya wateja inavyoongezeka.”

Anasema moja ya malengo aliyonayo ni kujifunza kutengeneza ubuyu huo ili kuhakikisha anawafikia wateja wengi zaidi wakiwamo wale wa jumla.

“Baadhi ya wateja huniuliza kama naweza kuuandaa (kuupika) lakini ukweli ni kwamba bado sijajifunza na hii ni kwa sababu kuna utofauti kati ya ubuyu wa embe unaopikwa hapa Dar es Salaam na ule unaopikwa Zanzibar,” anasema.

Mbali na kutengeneza ubuyu, Marry ana malengo ya kufungua duka la vyakula.