MAISHA NA MAHUSIANO: Dalili za mwanaume aliyemchoka mpenzi

Mwanaume anaanza kuonyesha hasira na kuhamaki kwa kila unachokifanya hata kama ni kitu kidogo. Hii ni kwasababu penzi limempungua au kumuisha na hivyo anakosa uvumilivu kwako. Anaweza kukupayukia hata ukiwa katikati ya watu, hatojali unavyojisikia kwa yeye kufanya hivyo. Utashangaa na kujiuliza mbona mwanzoni aliweza kunivumilia? Jibu ni kwamba penzi limepoa au kuisha

Dalili ya pili

Kwa kawaida mwanaume anavyompenda mwanamke huwa na kiu ya kumfurahisha, hufanya vitu kuhakikisha mpenzi wake anatabasamu na anajisikia murua. Kila siku kiu ya mwanaume ni kuona mwanamke anatamani kuendelea kuwa ndani ya penzi hilo. Mapenzi yakiisha vitu hivi vyote vinapeperukia mbali.

Dalili ya tatu

Mapenzi ya mwanaume yanapokwisha kwa mpenzi wake anakosa kabisa kuwa na muda naye. Mwanzoni mlikuwa mnakuwa na muda wa pamoja sasa hapati tena muda huo na kila ukiuliza visingizio kibao, mara kazi, ubize, mara safari, kuumwa au kuchoka n.k. Yaani inakuwa bora atumie muda wake akiwa na rafiki zake kuliko kuwa na wewe. Vicheko vya pamoja mkiwa peke yenu vyote vinakwisha. Ukiona hivyo jua hiyo taa nyekundu ndugu yangu

Dalili ya nne

Dalili hii yaweza kufanana kidogo na niliyokwishaisema. Mwanaume anapoacha kumpenda mwanamke hupunguza sana au kuacha kabisa kumjali na kumhudumia mpenzi wake. Inakuwa ngumu kwake kukufanya ujisikie mwanamke au ujisikie aalumu kwake. Atawatendea wengine mema na kuwajali lakini si wewe. Zile bashasha na malavidavi aliyowahi kuwanayo hutoyaona.

Dalili ya tano

Mapenzi ya mwanaume yanapopungua au kuisha kwako utaona jinsi inavyokuwa ngumu kuwasiliana na wewe. Unapomwonyesha umuhimu au uhitaji wako wa mawasiliano yeye anaona mzigo mkubwa. Anakuwa mzito kuzungumza, mgumu kuzionyesha hisia zake kwako, mara nyingine inakuwia ngumu kugundua lini amefurahi na lini amekasirika. Zamani alikusikiliza, sikuhizi hakusikilizi tena. Zamani ulijua alipo na anachofanya sikuhizi ukiuliza unazua ugomvi.

Dalili ya sita

Mwanaume anapompenda mwanamke humruhusu mwanamke huyo kuyajua maisha yake yote. Maisha ya mwanaume huyu yanakuwa kama kitabu kilichowazi. Hafichi kitu wala kuishi maisha ya kona kona. Tofauti yake ni kwamba mapenzi yakimwisha utaona siri zinakuwa nyingi, haujui nini kinaendelea kwenye maisha yake na wala haoni umuhimu wa kukushirikisha kinachoendelea kinachomhusu yeye.

Dalili ya saba

Penzi la mwanaume linapoisha juu yako mara nyingi huwa anaona shida kukushirikisha kwenye maisha yake au yeye kushiriki maisha yako. Furaha yake inakuwa yake na yako inabaki kuwa yako wakati mwanzoni furaha ya kwako ilikuwa furaha yake. Ukifanikiwa kitu na yeye anajisikia furaha lakini si sasa. Inapofikia hapa utaona mnakaa nyumba moja kama wapangaji wawili na si mtu na mwenza wake.