UREMBO: Fahamu jinsi ya kutumia mtindi kuondoa chunusi

Uso ni sehemu ya mwili inayopewa kipaumbele kuliko eneo lingine. Zipo njia nyingi za kuufanya uso uonekane mwororo siku zote.

Miongoni mwa njia hizo ni pamoja na kuukinga na chunusi kwa kutumia njia za asili na kuachana na za kemikali. Moja ya njia hizo ni kutumia mtindi.

Ikumbukwe kuwa maziwa ya mtindi kwa asili yake yana asidi nyingi, asidi ambayo ikitumika kwenye ngozi ni kinga dhidi ya bakteria na yale mafuta yanasaidia kuleta unyevunyevu na kuifanya ngozi kuteleza kama ya mtoto mdogo.

Namna ya kufanya ili kupata matokeo chanya, chukua kijiko kimoja cha chakula, cha asali, kiasi kama hicho cha mtindi. Changanya asali na mtindi uchanganyike vizuri. Halafu chukua kipande cha pamba chovya katika mchanganyiko huo na upake uso mzima.

Kaa kwa dakika 15 hadi 20, kisha sugua taratibu kuzunguka uso kabla hujauosha na maji safi. Mpaka hapo utakuwa umemaliza na unaweza kupaka mafuta unayotumia siku zote. Fanya hivi mara mbili kwa wiki kwa matokeo ya haraka.