ONGEA KILIMO : Inawezekana kujiajiri kwa kufuga nyuki

Muktasari:

Majike ya nyuki wadogo wote huzaa, huku madume yakifanya kazi kama nyuki wengine. Uzalishaji asali kwa nyuki wadogo hufanywa kwa ushirikiano.

Ufugaji wa nyuki umekuwepo kwa miaka mingi ambapo jamii mbalimbali zimekuwa zikifuga kwa njia za asili ili kujipatia chakula na kipato. Sasa ufugaji huo umeendelea kiteknolojia na kibiashara.

Kuna aina mbili za nyuki, wakubwa au maarufu kama nyuki wakali na wadogo. Watu wengi wamekuwa wakifuga yuki wakubwa kutona na urahisi wake kuwafuga tofauti na nyuki wadogo.

Nyuki wakubwa wanaweza kufugwa katika mapori, shambani, na hata katika nyumba maalumu ambazo hujengwa na kuwekwa mizinga kwa ajili ya kuzalisha asali kisasa. Nyuki wadogo kwanza ni wachache na uzalishaji wao wa asali ni mdogo, japo asali yao inauzwa kwa bei ya juu.

Majike ya nyuki wadogo wote huzaa, huku madume yakifanya kazi kama nyuki wengine. Uzalishaji asali kwa nyuki wadogo hufanywa kwa ushirikiano.

Asali inayotokana na nyuki hawa, ina aina nyingi zaidi za virutubisho kwa kuwa huweza kupata chavua kutoka katika aina mbalimbali za maua. Kutokana na maumbo yao huweza kuingia hata kwenye maua madogo ambayo nyuki wakubwa hawawezi kuingia.

Eneo linalofaa kufugia nyuki wakubwa ni lenye miti na uoto wenye mimea iwe ya mazao ya chakula au biashara, liwe na maji ya kudumu ambayo hutumika kama sehemu ya chakula cha jamii nzima ya kundi la nyuki.

Uoto wa miti yenye kivuli huwarahisishia nyuki katika ubebaji maji kwa ajili ya kupunguza joto. Wanatakiwa kufugwa mbali na makazi ya watu angalau mita 300 na lisiwe na wanyama wafugwao kama ng’ombe kwani ni maadui wa nyuki. Eneo hilo pia linaweza kurahisisha mawasiliano ya watu wanaohudumia shamba hilo.

Mizinga

Nyuki huishi na kufanya kazi kwenye viota wanavyojenga katika magome ya miti, miamba na mapango. Hata hivyo, kwa wafugaji, wamekuwa wakijenga mizinga ili kuwavutia nyuki ili kuzalisha asali.

Kuna mizinga ya asili na mizinga ya kisasa. Mizinga ya asili ni magogo, magome, vikapu, vyungu au matete. Faifda ya mizinga ya asilini ni gharama nafuu kwa kuwa inapatikana kwenye mazingira ya porini. Tatizo lake ni rahisi kuharibika wakati wa ukaguzi na uvunaji wa asali na hutumia muda mwingi wakati wa uvunaji.

Mizinga ya kisasa ipo ya aina mbili; mizinga ya kati na ya biashara. Mizinga ya kati huwa katika mfano wa sanduku, vipimo vyake hutegemea matakwa ya mfugaji.